27 May 2013

CUF yatoa tamko la udini

Na Reuben Kagaruki


 CHAMA cha Wananchi (CUF), kimesema kitaendelea kuwalaani kwa nguvu zote watu wanaotaka kuwagawa Watanzania, wawe ni viongozi au wananchi kwa misingi ya dini zao.
Taarifa iliyotolewa na chama hicho kwa vyombo vya habari Dar es Salaam jana, ilisema hivi karibuni gazeti moja (si Majira), liliandika habari iliyomhusisha Mwenyekiti wa CUF Taifa, Profesa Ibrahim Lipumba na masuala ya udini.
Katika taarifa hiyo, CUF kimeitaka Wizara ya Habari, Vijana Utamaduni na Michezo, kutovifumbia macho baadhi ya vyombo vya habari ambavyo vinataka kuwapeleka Watanzania kusiko hasa kipindi hiki ambacho nchi imegubikwa na matukio mengi yanayohusu migongano ya
dini na kusababisha uharibifu katika nyumba za ibada.
“Tunasisitiza na kulaani uandishi wa aina hii, tutaendelea kulaani wale wanaolenga kuwagawa Watanzania wawe ni viongozi au wananchi kwa misingi ya dini zao,” ilisisitiza taarifa hiyo.
Chama hicho kiliongeza kuwa, magazeti ya aina hiyo yamekuwa yakichochea uhasama wa kidini na kuwabagua wananchi kwa mujibu wa imani zao yakihusishwa na uchochezi huo na baadhi ya vyama vya kisiasa pamoja na viongozi wake.
“Tumeshangazwa na tuhuma za udini kuelekezwa kwa Mwenyekiti wetu Taifa...hii inaonesha uandikaji habari wa aina hii una lengo la kuvigawa vyama vya siasa kwa falsafa ya udini,” iliongeza taarifa hiyo.
Kimesema hali halisi ya habari hiyo ni kutaka kuonesha kwa wananchi kuwa Prof. Lipumba na Rais Jakaya Kikwete kila mmoja akiwa ni Mwenyekiti wa chama cha siasa, waligubikwa na imani za udini katika kampeni zao kwa kutegemea kura za Waislamu.
Taarifa hiyo ilisema kuwa, habari hiyo ilikwenda mbali zaidi na kusema kuwa, “Prof. Lipumba amekuwa akitumia misikiti na viongozi wa dini hiyo ili Waislamu nchini waendelee kukiunga mkono chama chake hasa katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015.
“Chama chetu hakiwezi kumzuia Prof. Lipumba, asihudhurie ibada katika msikiti wowote anaotaka, kualikwa kanisani au kwenye mahekalu ya Kihindu,” ilisema taarifa hiyo.
Iliongeza kuwa, CUF kinatambua kuwa Prof. Lipumba ni Muislamu hivyo chama hakiwezi kumzuia asihudhurie ibada kwenye Msikiti na sehemu nyingine ambazo ataalikwa na kutakiwa kutoa hotoba kwa waumini au waliomualika.
“Kumbukumbu zinaonesha Rais wa Awamu ya Tatu, Bw. Benjamin Mkapa wakati akiwa madarakani alitangaza kuwapa Waislamu Chuo cha Shirika la Umeme nchini (TANESCO), kilichopo mkoani Morogoro na kuwa Chuo Kikuu cha Kiislamu.
“Si vibaya kwa Prof. Ibrahim Lipumba kutoa kauli ya kuwataka Waislamu wajipange katika ibada aliyoalikwa,” ilifafanua taarifa hiyo.

No comments:

Post a Comment