27 May 2013

MCT sasa wamshukia Nkamia

Na Darlin Said


 BARAZA la Habari nchini (MCT), limesema halitatetereka kupigania haki za waandishi wa habari badala yake wataendelea kusimamia weledi, maadili na maendeleo ya kitaaluma kupitia programu mbalimbali.
 Katibu Mtendaji wa MCT, Bw. Kajubi Mukajanga, aliyasema hayo Dar es Salaam jana wakati akizungumza na waandishi wa habari wakati akitoa ufafanuzi wa kauli iliyotolewa na Mbunge wa Kondoa Kusini, Bw. Juma Nkamia (CCM), kuwa baraza hilo na Jukwaa la Wahariri nchini (TEF), ni taasisi NGOs zenye masilahi binafsi.
Bw. Nkamia alitoa kauli hiyo bungeni mjini Dodoma hivi karibuni wakati akichangia mjadala wa Bajeti ya Wizara Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo.
Kutokana na kauli hiyo, Bw. Mukajanga alisema baraza hilo limesikitishwa
na kauli hiyo yenye lengo la kukwamisha kazi zao kwa uhuru.
“Kauli hii ina nia mbaya kwa ustawi wa baraza huru ambalo limefanikiwa sana katika Kanda ya Afrika, MCT haipo tayari kuona kazi nzuri iliyofanywa kwa miongo miwili ikanyagwe, kuupuzwa na watu wachache.
“Historia ya Baraza inajieleza yenyewe kwani lilianzishwa na wanahabari wenyewe mwaka 1995 baada ya kupinga mpango wa Serikali iliyotaka kuweka sheria mbaya ya kudhibiti vyombo vya habari,” alisema Bw. Mukajanga.
Alisema wakati Bw. Nkamia akiwa Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Maendeleo ya Jamii, aliongoza ujumbe wa wabunge na wajumbe wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar, kwenye ziara ya mafunzo nchini India mwaka 2011.
Aliongeza kuwa, safari hiyo iliandaliwa na MCT ili wabunge na wawakilishi waende kujifunza jinsi Sheria ya Haki ya Kupata Habari ilivyokuwa inafanya kazi.
“Katika safari hile, Bw. Nkamia aliongea mambo mazuri kuhusu jitihada za wadau wa habari; iweje leo hii awe msaliti, tunaomba kauli yake iliyojaa dharau ipuuzwe,” alisema.

No comments:

Post a Comment