27 May 2013

CCM, CWT Bunda wavutana kiutendaji

Na Raphael Okello, Bunda


 KATIBU Mwenezi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Wilaya ya Bunda, mkoani Mara Jonas Sariro, ametoa onyo kwa viongozi wa Chama cha Walimu nchini (CWT), wilayani humo na kudai kuwa, CCM ina jukumu la kuwasimamia watumishi wa Serikali ili waweze kutekeleza sera na ilani ya chama.
Sariro ametoa onyo hilo kutokana na madai ya CWT wilayani humo kuilalamikia CCM wakidai viongozi wake wanafanya kazi za Serikali kwa kukagua utendaji wa walimu shuleni, kuwafokea na kutishia kuwafukuza kazi au kuwahamisha.
CWT walidai kuwa, hoja ya viongozi wa CCM ni juu ya chama ambacho ndicho kinachoongoza dola kuwajibika kuwalipa mishshara walimu.
Alisema CCM ipo tayari kuwachukulia hatua walimu wote ambao
watashindwa kuwajibika na kuwataka viongozi wa CWT waache kuwapotosha wanachama wao (walimu).
Akizungumza na waandishi wa habari mwishoni mwa wiki, Sariro alisema madai ya CWT hayana maana kwani Mwenyekiti wa CCM wilayani humu, Bw. Chacha Gimanu, yuko katika ziara ya kuangalia utekelezaji wa ilani ya uchaguzi.
Aliongeza kuwa, ziara hiyo inafanyika katika kata zote wilayani hamo ili kutoa mapendekezo mbalimbali katika maeneo ambayo yatabainika kuwa na kasoro za kiutendaji si kutoa vitisho.
“Katika ziara hizi, Ofisa Mtendaji wa kata ambaye ndiye Katibu wa Kamati ya Maendeleo ya kata, husoma taarifa ya utekelezaji wa ilani akisaidiana na wakuu wa idara mbalimbali katika kata ikiwemo idara ya elimu.“Sisi hatuwahoji walimu kama inavyodaiwa, CWT inataka kuacha malengo yake na kugeuka kuwa chama cha siasa.
Naomba chama hiki kisimamie wanachama wake ili wawajibike ndipo wadai masilahi yao,” alisema.
Hivi karibuni, Mwenyekiti wa CWT wilayani humo, Bw. Francis Ruhumbika, aliituhumu CCM kuwa Mei 22 mwaka huu, Mwenyekiti wake wa Wilaya, Bw. Gimanu alifika katika Shule ya Msingi Nyamuswa ‘A’, kuwaita walimu, kuwahoji na kuwatishia kuwa atawahamisha vituo vya kazi.
“Sisi viongozi wa CWT wilaya ya Bunda tunasema kuwa, Mwenyekiti wa CCM wilayani hapa si mamlaka ya nidhamu ya walimu...viongozi wa kisiasa wafanye mambo ya siasa,wasigeuke kuwa mamlaka ya kuwajibisha walimu,” alisema.

No comments:

Post a Comment