08 February 2013

Mwenyekiti CUF jela miezi 16



Na Steven Augustino, Tunduru

MWENTEKITI wa Kata ya Nakapanya, Wilaya ya Tunduru,
mkoani Ruvuma kwa tiketi ya Chama cha Wananchi CUF, Bw. Hassan Sinda, amehukumiwa kifungo cha miezi 16 jela baada
ya kupatikana na hatia ya uchochezi na kutishia kuua.


Hukumu hiyo imetolewa na Mahakama ya Mwanzo Milingoti
mjini humo baada ya kutiwa hatiani kwa kosa kla kutishia
kumuua diwani ya kata hiyo, Mfaume Wadali na kutoa
tamko la kuwazuia wananchi kufanya kazi ya kujitolea.

Kesi hiyo ya jinai namba 21/2011, ilihusu makosa ya kutishia kuua kwa maneno kinyume na kifungu cha Sheria namba 89 (2) (C) sula ya 16 cha kanuni ya adhabu na jinai namba 20/2011 ya kuwazuwia wananchi kusijitolee katika shughuli za maendeleo kinyume cha kifungu cha Sheria namba 89 (2) (C) sula ya 16 cha kanuni ya adhabu.

Hakimu wa Mahakama hiyo, Abdalah Mponda alisema baada
ya mahakama kupitia kanuni, vipengere vya sheria na kusikiliza ushahidi uliotolewa, imemtia hatiani mshtakiwa na kutoa hukumu
ya kutumikia miezi minne jela au kulipa faini ya sh. 200,000 kwa
kosa la kutishia kwa maneno.


Kwa upande wa kosa la jinai la kushawishi wananchi wa kata hiyo kutoshiriki shughuli za maendeleo, mahakama hiyo imeona ili iwe fundisho kwa viongozi wengine wanaoona siasa ni sehemu ya kudidimiza maendeleo kwa wananchi, mshtakiwa alihukumiwa
kifungo cha miezi 12 jula bila faini.

Mahakama hiyo imetoa mwezi mmoja kwa mshtakiwa kukata rufaa katika Mahakama ya Wilaya kama hajaridhika na hukumu.

Awali Hakimu Mponda alidai kuwa, mshtakiwa alitoa maneno
hayo katika mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye Viwanja
vya Chekechea vilivyopo kwenye Shule ya Msingi Nakapanya
Oktoba 26,2011 na kufunguliwa mashtaka Oktoba 28,2011.

Baada ya kupewa nafasi ya kujitetea, mshtakiwa ambaye pia
alikuwa Mwenyekiti wa Serikali ya Kijiji cha Nakapanya
aliiomba mahakama hiyo impunguzie adhabu kwa sababu
ya kusumbuliwa na maradhi kama Kifua Kikuu, kisukari,
moyo pia anategemewa na watoto wanne anaowasomesha
pamoja na mama yake mzazi ambaye ni mzee sana.

No comments:

Post a Comment