21 February 2013

Brandts: Azam njia ya ubingwa



Na Elizabeth Mayemba

KOCHA Mkuu wa Yanga, Ernest Brandts amesema endapo timu yake itawafunga Azam FC mechi yao ya Ligi Kuu, Jumamosi watakuwa wamejisafishia njia ya kutwaa ubingwa.

Akizungumza na gazeti hili Dar es Salaam jana, Brandts alisema kwa sasa wapinzani wao kuelekea kwenye ubingwa ni Azam FC, hivyo wakiwafunga Jumamosi watakuwa wamewapunguzia kasi ya ubingwa.

"Azam ni timu ambayo ndiyo tunafukuzana nayo kwenye ubingwa, hivyo tukiwafunga Jumamosi tutakuwa tumejisafishia njia kuelekea kwenye ubingwa, na ndiyo maana nimekuwa mkali mazoezini ili wachezaji wangu wasiwe wazembe," alisema Brandts.

Alisema mzunguko huu ni wa lala salama, hivyo kila timu inataka kuhakikisha inashinda kila mchezo, wapo ambao wanajiweka katika mazingira ya kutoshuka daraja na nyingine kuwania ubingwa, hivyo atahakikisha hafanyi kosa kwenye kila mchezo watakaocheza.

Kocha huyo raia wa Uholanzi, alisema wachezaji wake wote wapo katika hali nzuri kiafya na wameahidi kufanya vizuri kwenye mechi zote za mzunguko huu na si kuangalia mechi moja tu.

Ili kuhakikisha timu hiyo inashinda mchezo wake wa Jumamosi dhidi ya Azam FC, juzi timu hiyo ilikwenda kuweka kambi Bagamoyo mkoa wa Pwani kutokana na upinzani mkali uliopo baina ya timu hizo mbili.

Brandts alisema anaamini kambi hiyo kwa kiasi kikubwa itawasaidia wachezaji wake, kwani muda wote watakuwa pamoja na kwa upande wake atapata nafasi nzuri ya kurekebisha kasoro ndogo ndogo

No comments:

Post a Comment