03 January 2013

Wanafunzi 1,466 Dar wakwama kufanya mtihani kwa utoro,vifo



Na Heri Shaaban

WANAFUNZI 1,466 wameshindwa kufanya mtihani wa darasa
la saba mwaka huu katika shule mbalimbali jijini Dar es Salaam kutokana na utoro pamoja na vifo.

Katibu Tawala wa Mkoa huo, Bi. Theresia Mmbando, aliyasema hayo jana wakati akizungumza na waandishi wa habari.

Alisema wanafunzi 20 walifariki dunia, ugonjwa 33 na wengine 1,597 sawa na asilimia tatu, hawakufanya mtihani huo kutokana
na utoro pamoja na sababu nyingine.

“Wanafunzi 58,093 ndio waliosajiliwa kufanya mtihani huo kati
yao, wasichana 30,494, wavulana 27,599, sawa na asilimia 97,” alisema Bi. Mmbando

Aliongeza kuwa, mwaka huu wanafunzi waliofaulu mtihani huo
ni asilimia 88.54, ambapo kiwango hicho kimepanda sawa na asilimia 10 ambapo chaguo la kwanza la wanafunzi waliofaulu
ni 11,677 na waliobaki watachaguliwa katika awamu ya pili
baada ya vyumba vya madarasa 292 kukamilika.

Aliwaagiza Watendaji wa Halmashauri za Mkoa huo kusimamia ujenzi wa vyumba hivyo na baada ya kukalimika, watoe taarifa
ili waweze kukamilisha chaguo la pili la wanafunzi.

Alisema upungufu wa vyumba hivyo kwa upande wa Ilala ni 70, Temeke 98, Kinondoni 124 na madawati 12,000 ambayo yanahitajika.

No comments:

Post a Comment