26 November 2012

Halmashauri Korogwe yashtakiwa CCM



Na Yusuph Mussa, Korogwe

MKUU wa Wilaya ya Korogwe Bw. Mrisho Gambo ameishitaki Halmashauri ya Mji wa Korogwe kwa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kuwa inanyanyasa wabeba abiria kwa njia ya pikipiki maarufu kama bodaboda pamoja na mamalishe.


Aliyasema hayo juzi kwenye mkutano wa Halmashauri Kuu ya CCM Wilaya ya Korogwe Mjini ambayo iliketi kwa ajili ya kuwapata wajumbe wa Kamati ya Siasa (CC ya Wilaya).

Bw. Gambo alisema kipato cha bodaboda ni kidogo, lakini halmashauri imeendelea kuwakamu kwa kuwataka walipe sh.500 kila siku wakati tayari wanalipa kwa mwaka sh. 35,000, na kuwataka halmashauri watafute vyanzo vingine vya mapato, lakini sio bodaboda.

"Vijana wengi wa bodaboda pikipiki sio zao bali wameajiriwa. Mwisho wa siku wanatakiwa kupeleka kwa tajiri sh. 6,000, lakini wakati huo huo na yeye anatakiwa kubaki na chochote kwa ajili ya familia yake, bado halmashauri inamtaka alipe sh.
500 kwa siku.

"Tayari bodaboda huyo analipa TRA sh. 35,000 kwa mwaka. Halmashauri tafuteni vyanzo vingine vya fedha. Tatizo la bodaboda wakati wa uchaguzi
linabadilika kuwa la kisiasa,"alisema.

Bw. Gambo alisema pia halmashauri inawanyanyasa na kuwaletea usumbufu akina mama wanaouza chakula maarufu kama Mamalishe kwa kusema pamoja na kwamba halmashauri wanataka wavae sare, lakini waweke muundo mzuri ambao hautawasumbua.

Alisema makosa yanayofanywa na watendaji kwenye halmashauri pamoja na viongozi wa kisiasa waliochaguliwa na wananchi kama wabunge na madiwani, lakini wakashindwa kuwajibika kwa wananchi  ni tishio kwa CCM Uchaguzi wa Serikali za Mitaa 2014 na Uchaguzi Mkuu 2015.



No comments:

Post a Comment