27 August 2012

Nyota wa kikapu NBA akoshwa na vipaji nchini



Na Amina Athumani

NYOTA wa timu ya mpira wa kikapu ya Chicago Bulls inayocheza Ligi Kuu ya mchezo huo Marekani (NBA), Luo Deng ameridhishwa na uwezo wa chipukizi wa Tanzania baada ya kuwaona katika kliniki inayoendeshwa na Mtanzania, Hashim Thabit anayechezea ligi hiyo pia.

Akidhihirisha kukoshwa na vipaji vya wachezaji hao, Deng alisema Dar es Salaam juzi, kwamba cha msingi  wachezaji hao wanapaswa kukizingatia ni kuongeza bidii kwani wanao uwezo mkubwa wa kupata nafasi ya kimasomo nje ya nchi na kujifunza zaidi mchezo huo kimataifa.

Alisema wachezaji wengi wazuri ambao wanaziwakilisha nchi zao katika medani ya kimataifa kama alivyo kwa Thabit na wengine kutoka mataifa mbalimbali, wamekuwa wakizingatia zaidi juhudi katika mchezo sambamba na masomo vitu ambavyo vimeweza kuwafikisha mbali na kuonekana kuwa ni tegemeo kubwa kwa klabu wanazozichezea na taifa lao kwa ujumla.

Naye Thabit alisema tangu kuanza kukutana na vijana katika kliniki zilizopita, hiyo ya sasa ina vipaji zaidi na kuridhishwa na ameridhishwa na uwezo wanaouonesha vijana hao, hivyo kuitabiria makubwanchi katika mchezo huo.

Kwa upande wake, Makamu wa Rais wa Shirikisho la Mpira wa Kikapu Tanzania (TBF), Phares Magessa alisema Kliniki hizo za Thabit zimekuwa na manufaa makubwa hasa ikihamasisha vijana kuupenda mchezo huu huku wakijituma na kuamini siku moja watakuwa wachezaji wazuri na tegemeo kwa taifa lao.

Alisema kilini hiyo pia imefanikisha kutoa mwanga kwa wachezaji wengi ambao wao kama TBF wanaamini watafuata nyayo za Thabit kama zilivyoanza kuonekana kwa mchezaji Alphaeus Kisusi ambaye yupo nchini Canada kimasomo kupitia mpira wa kikapu.

Kliniki hiyo ilifanyika juzi katika viwanja vya Donbosco, Upanga, Dar es Salaam ilishirikisha vijana wadogo huku ikisimamiwa na shirikisho hilo.

No comments:

Post a Comment