29 August 2012

Mfadhili CHADEMA ahamia CCM



Na Faida Muyomba, Sengerema
 
MLEZI na Mfadhili Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Jimbo la Sengerema, mkoani Mwanza, Bw. Alex Manji, ametangaza rasmi kukihama chama hicho na kujiunga Chama Cha Mapinduzi (CCM).

 
Bw. Manji ambaye hivi karibuni alitangaza kuwania ubunge wa jimbo hilo kwa tiketi ya CHADEMA, katika Uchaguzi Mkuu ujao, alifikia uamuzi huo kwenye Mkutano Mkuu wa Uchaguzi Jumuiya ya Wazazi wa CCM, wilayani hapa, uliofanyia jana.

Alisema hajashawishiwa na mtu kukihama chama hicho bali amebaini kuwa kuendelea kukaa huko ni sawa na kupoteza muda wake kwani CCM ndio chama kilichomlea tangu utoto wake.

“Nimeamua kurudi nyumbani CCM kwa hiari yangu, nitakuwa bega kwa bega na wanachama wote kuhakikisha tunaisambaratisha CHADEMA hapa Sengerema.

“Ninaijua vizuri CHADEMA kwa sababu nimekuwa mdhamini wao mkuu katika jimbo hili,’’ alisema Bw. Manji ambaye pia alikuwa Mwenyekiti wa chama hicho Kata ya Nyampulukano.
 
Katika mkutano huo, Bw. Manji alipewa kadi yenye namba 0136371 iliyotolewa Novemba 5,2010, na mgeni rasmi Kamanda wa Vijana wa CCM wilayani hapa, Bw. William Ngeleja, ambaye alisema uamuzi aliochukua ni wa busara na unastahili kupongezwa.
 
Akizungumzia uchaguzi huo, Mbunge wa jimbo hilo, Bw. William Ngeleja, aliwataka wajumbe wa mkutano huo kuchagua viongozi ambao watasaidia kuimarisha chama katika Uchaguzi Mkuu ujao.
 
“Ndugu wajumbe, naomba tuwe makini tunapochagua viongozi ambao watakuwa msingi imara wa chama chetu huko tunakokwenda ili tuendelee kuwatumikia wananchi,” alisema.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa CCM wilayani humo, Bw. Jaji Tasinga, aliwataka wajumbe wa mkutano huo wajitokeze kwa wingi kutoa maoni yao kwenye tume ya kukusanya maoni ya Katiba Mpya.
 

3 comments:

  1. M4C itadumu tu daima. Hii ni special kwa vijana wasomi wanaohitimu vyuo sasa na kutaka mageuzi, yawe mazuri au mabaya, kinachotakiwa ni mageuzi tu hata akihama Dr. Slaa. Moto umeshawashwa na hamna zima moto,unawaka tu taratibu mwisho mtakuja uona,kama ilivyokuwa Zambia,Kenya,Tunisia na kwingineko.

    ReplyDelete
    Replies
    1. Mbona huutaji moto wa LIBYA? Kumbuka kwamba moto ukianza kuwaka hauchagui huyu ni M4C, CDM au CCM!! Unchoma wote!!!!! Halafu kumbuka pia, sio M4C peke yao wenye monopoly au turufu ya kowasha moto. Hata wengine pia wanao uwezo huo wa kuwasha moto, tena sana tu!! Nivyema kuwa mwangalifu, kwa vile mioto kama hiyo ya M4C inaendelea kuwaka Libya, Iraq na Syria, na kama usemavyo, hakuna zimamoto. Siku hiyoo, sijuli lini, moto utapozimika kwa kukosa kuni hakuna uhakika nani atakuwa amebaki, na hata akibaki, ataambulia majivu ya kile alichodhani anakipigania. Waulize Ivory Coast, Abidjan ilikuwa Paris ya Afrika! Iko wapi leo? Moto ukianza. kwa kuwa hauna zimamoto, si rahisi sana kujua utazimikia wapi na lini!

      Delete
  2. hawa ndiyo mamluki ambao Chadema hawawahitaji. eti kadi yake ilitolewa 5 novemba 2010. yaani alikua anasubiri nini kama siyo kukidadisi chama kwa manufaa ya ccm? chama siyo mtu moja kwani jogoo moja akisusia kuwika hakuwezi kuzuia jua kujotokeza

    ReplyDelete