27 August 2012

Karani wa sensa auawa, aporwa fedha sh. 200,000



Na Patrick Mabula, Kahama

KARANI wa sensa ambaye ni Mwalimu wa Shule ya Msingi Kawe, iliyopo Kata ya Kilago, Wilaya ya Kahama, mkoani Shinyanga, Stanley Mahene, ameuawa na watu wasiofahamika na kuporwa sh.200,000, alizolipwa baada ya kuhudhuria mafunzo ya sensa.


Tukio hilo lilitokea juzi baada ya watu wanaodhaniwa kuwa majambazi, kuvamia nyumbani kwake, kuvunja mlango, kuingia ndani, kumkata kwa mapanga sehemu mbalimbali za mwili, kupora fedha hizo na mali nyingine.

Kamanda wa Polisi mkoani hapa, Evelist Mangalla, alithibitisha kutokea kwa tukio hilo kijijini hapo.

“Marehemu alirudi nyumbani kwake akiwa na fedha hizo lakini watu wasiofahamika walivamia nyumba yake, kumpiga mapanga, kumpora fedha na mali nyingine,” alisema Kamanda Mangalla.

Aliongeza kuwa, vitu vingine walivyochukua watu hao ni pamoja na simu ya mkononi, televisheni, jenereta pamoja na deki ambapo hadi sasa, Jeshi la Polisi linawashikilia watu watatu kwa tuhuma za kuhusika na mauaji hayo baada ya kukamatwa na baadhi ya vitu vilivyoibwa kwa marehemu.




No comments:

Post a Comment