09 July 2012
Watalii 50,000 wajitokeza uzinduzi wa ZIFF
Na Amina Athumani, Zanzibar
WATALII zaidi ya 50,000 wamejitokeza katika uzinduzi wa tamasha la 15 la Kimataifa la Filamu za Nchi za Majahazi ambalo hufanyika Zanzibar kila mwaka (ZIFF).
Tamasha hilo limezinduliwa juzi katika mji wa Ngome Kongwe, Zanzibar na kushirikisha wasanii, watayarishaji na waongozaji pamoja na wadau wengine kutoka nchi mbalimbali Dauniani.
Akizungumza mjini hapa wakati wa uzinduzi wa tamasha hilo, Mkurugenzi Mkuu wa ZIFF,Profesa Ikaweba Bunting aliwashukuru wadau mbalimbali kwa kuwaunga mkono kila mwaka tangu kuanza kwa tamasha la kwanza mpaka la sasa ambapo linatimiza kipindi cha miaka 15.
“Tunawashukuru Wazanzibar na wageni wote kwa kuwa nasi bega kwa bega kila mwaka katika tamasha hili ambalo limekua chachu kubwa ya maendeleo na mambo mbalimbali katika msimu huu wa tamasha, hivyo tunajisikia faraja kwa kuungwa mkono” alisema Ikaweba.
Pia aliwashukuru Kampuni ya Wananchi Group, inayomiliki ving’amuzi vya ZUKU ambao wamedhamini tamasha hilo kwa dola za kimarekani milioni moja kwa miaka 10.
Tamasha hilo lilifunguliwa na mgeni rasmi, Mkurugenzi Mkuu wa Kamisheni ya Utalii Zanzibar, Ali Khalil Mirza ambaye alilipongeza tamasha hilo kwa ukomavu wake visiwani Zanzibar na kuchangia pato kubwa la ongezeko la utalii na wageni mbalimbali wakati wa msimu.
Kwa upande wake, Mwenyekiti mpya wa ZIFF, Mohmoud Thabit Kombo aliwashukuru ZUKU kwa udhamini wao huo huku akitoa fursa na kwa kampuni nyingine kujitokeza kudhamini ilikufikia malengo zaidi ambayo yanafanywa kila mwaka na Tamasha.
Naye, Mwenyekiti wa Wananchi Group, Ali Mufuruki alisema tamasha hilo la ZIFF lina fursa ya kipekee kwa hapa nchini na wataendelea kushikamana bega kwa bega katika kufikia malengo ikiwemo kuendeleza sanaa mbalimbali sambamba na kusambaza kila mahali huduma za ZUKU hapa nchini.
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment