31 July 2012

Migogoro ya ardhi inakwamisha maendeleo

Na Grace Ndossa

MIGOGORO ya ardhi ambayo inaibuka mara kwa mara inachangia kwa kiasi kikubwa kurudisha nyuma maendeleo ya sekta ya kilimo na kuendelea kuangamiza zaidi ya asilimia 70 ya watanzania ambao huishi kwa kutegemea kilimo.

Hali hii inatokana na ukweli kuwa zaidi ya watanzania wanategemea kukuza uchumi wao kupitia kilimo ambacho hutegemea ardhi.

Sambamba na kilimo pia jamii kubwa ya wananachi hutegemea ardhi kwa ajili ya kufuga mifugo yao na kujipatia mahitaji yao ya kila siku.

Hali ya kuwepo kwa migogoro ya ardhi ya mara kwa mara katika sehemu mbali mbali za  Tanzania inachangia kwa kiasi kikubwa kurudisha nyuma ufanisi katika sekta za kilimo na mifugo na kusababisha kurudisha nyuma maendeleo  ya wananchi.

Akizungumza na waandishi wa habari hivi karibuni Mkurugenzi wa taasisi ya utafiti ya kutetea Haki za Ardhi Bw. Yefred Miyenzi anasema kuwa  kutokana na utafiti waliofanya mji wa kigamboni  tangu  serikali  ilipobuni mradi wa  kuanzisha  mji mpya mwaka2008 wamebaini athari mbali mbali zilizotokea tangu  kusitishwa kwa shughuli za  kiuchumi na kijamii.

Anasema kuwa kutokana na hali hiyo waliamua kufanya utafiti maalum juu ya athari , kijamii na  kimazingira zilizotokana  na kuanzishwa kwa mradi huo tangu 2008 hadi sasa na athari za kimazingira endapo hali hiyo haitarekebishwa kutokana na matokeo ya utafiti huo.

Anaelezea kuwa utafiti huo uliongozwa na  Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Tumaini Kampasi ya Dar es salaam  Profesa  Sist Joseph  akishirikiana na  Bi Rosemary Mramba kutoka Taasisi ya ushauri  wa masuala ya maendeleo na jamii (FOSSTAN).

Bw. Miyenzi anasema kuwa utafiti huo  ulianza Disemba mwaka jana  hadi Machi 2012 ulioshirikisha watu mbali mbali wakiwemo ngazi za  serikali za mitaa kata na halmashauri husika wananchi wa kigamboni Ofisi iliyoratibu mradi huo katika Wizara ya Ardhi.

Anasema kuwa  utafiti huo ulibaini kuwa  shughuli za uchumi  zimesimama kwa muda mrefu  na kusababisha wananchi wanaotegemea kilimo upandaji wa  mihogo  mbogamboga  kudorora na nyingine kufa kabisa na hivyo kuathiri kipato kwa kaya zilizokuwa zikijikimu kutokana na shughuli hizo.

Pia anasema kuwa  kukosekana kwa mikopo kutoka taasisi za kifedha kwa dhamana ya mali kwani wananchi walio wengi walikuwa wanatumia ardhi yao kuweka  rehani ili waweze kupata mikopo na kuendeleza shughuli za kiuchumi pamoja na kusomesha watoto  lakini tangu kusitishwa kwa shughuli hicho maisha yao yameyumba kiuchumi.

Hata hivyo anasema kuwa tangu kutolewa kwa  tamko hilo  kasi ya  wapangaji wa makazi  imekuwa ikipungua wakiwa na imani  kuwa mradi unaweza kuanza  muda wowote na wapangaji wanapopatikana hawakubali  mikataba ya muda mrefu na badala yake hulipa kodi ya pango ya mwezi mmoja

Bw. Miyenzi anasema kuwa tangu tamko hilo litolewe la kusitisha  maendeleo katika eneo  la mradi kigamboni  ilikuwa inakua kwa kasi kutokana na ujenzi wa majengo mapya  hasa kwa ajili ya makazi

Pia  utafiti huo ulibaini kuwa baadhi ya majengo ambayo watu walikuwa  wakijenga kabla ya kutolewa kwa amri ya zuio yamebaki bila ya kuyaendelezwa, hii imeathiri kwa kiasi kikubwa mategemeo ya wananchi ya kujipatia kipato endapo wangeweza kumaliza majengo yao.

Hata hivyo vijana wengi wamekosa fursa za ajira bila ya kuwa na njia mbadala  ya kupata kipato kwani hii inachangi idadi kubwa ya vijana kujiingiza katika matukio na matendo ya  uvunjaji wa sheria kama vile  uporaji , ukabaji na matumizi ya madawa ya kulevya.

 Anasema kuwa mzunguko wa kifedha umepungua kutokana kupungua kwa shughuli za uzalishaji pamoja na wategemezi wa shughuli za msingi za kiuchumi pamoja na  wauzaji wa vyakula  kwa wafanyakazi .

Bw. Miyenzi anasema kuwa  kumekuwapo na athari za  kisaikolojia kwa baadhi ya wakazi wa Kigamboni kwani jamii imeshindwa kutabiri nini hatima yao majengo ambayo hayajakamilika watu hawana vipato vya  kujikimu hawajui fidia itatoka lini, kutokana na mfumo wa uthamini  hauko wazi na taarifa haziwafikii kwa wakati.

Katika utafiti huo  wakazi wa kigamboni walieleza kuwa serikali  haijawa wazi na wananchi wa eneo hilo hawajui  faida ya huo mradi kwao  na bado wana hofu ya kuwa wageni  katika ardhi yao na kutaka kujua nini wajibu wao na kwa muda gani wakae wakisubiri.

Wanaeleza kuwa  baada ya  amri ya zuio kuisha muda wake baada ya miaka miwili hakujawa na taarifa za wazi kuwaambia nini kinachoendelea licha ya kusikia tu mijadala bungeni na kwenye vyombo vya habari kwani kinachotakiwa ni  uwazi katika kutekeleza mradi hatua kwa hatua badala ya kuwaacha wananchi wakipiga ramli kubashiri nini kitatokea.

Pia anasema kuwa wakazi  wa kigamboni  wanahitaji kushirikishwa kikamilifu  kujadili na kutoa  mawazo yao kwa njia ya vikao halali kama  wamiliki wa  ardhi sheria ya mipango miji inawatambua kama wadau muhimu na kama siyo serikali inayotaka kuwekeza kwanini wawekezaji  wasingekwenda wao wenyewe moja kwa moja  kujadili na  wananchi.

Anasema kuwa malipo ya fidia  kamili na ya haki  kwa wakati  anaeleza kuwa  uzoefu unaonesha  kuwa katika miradi mingine  kuwekuwa na tatizo la ulipwaji fidia kwani wananchi wanataka kuona zoezi la uthaminishaji mali na rasilimali zao linakuwa na wazi  na ushirikishwaji unatakiwa  ili hatimaye fidia iweze kuwa ya haki  kulingana na  viwango vya soko.

Hata hivyo anasema kuwa kuna haja  ya kuangalia  fidia ilipwe kwa kuzingatia bei ya soko lililopo hivi sasa badala ya kufanya tathimini kwa kutumia bei ya zamani ambayo inaangali thamani ya wakati huo ya sarafu .

Bw.Miyenzi anasema kuwa  kutokana na utafiti huo  madai ya wananchi kutokana na  matokeo ya utafiti huu yazingatiwe na  kufanyiwa kazi ili haki itendeke na wananchi wasibaki kuwa wahanga wa maendeleo  badala ya kunufaika nayo, Suala la ushirikishwaji wa wananchi katika kila hatua linapaswa kupewa kipaumbile kwani kukosekana kwake ndicho kiini cha migogoro mingi ya ardhi isiyokwisha mijini na vijijini.

Pia serikali inatakiwa kujenga utamaduni wa kuheshimu haki za wenyeji kwenye ardhi  badala ya mara zote kuwachukulia kama watu wasio stahiki wakati wamewekeza  nguvu kazi zao  mali na rasilimali zao na  fidia itazamwe upya badala ya kutolewa kwa mkupuo mara moja inaweza kutolewa kwa awamu na kushirikisha vitu visivyo  pesa taslimu kama vile ubia katika miradi.

No comments:

Post a Comment