29 June 2012

Kesi ya UDA yakwama kusikilizwa



Na Rehema Mohamed

MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam, jana ilishindwa kupanga tarehe ya kuwasomea maelezo ya awali washtakiwa wa kesi ya kughushi, kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu na kulisababishia hasara Shirika la Usafirisha Dar es Salaam (UDA), sh. billion 2.3, kutokana na mshtakiwa wa pili kutokuwepo mahakamani.

Kesi hiyo inamkabili aliyekuwa Waziri wa Zamani wa Viwanda na Biashara, Bw. Iddi Simba, Meneja Mkuu wa shirika hilo, Bw. Victor Milanzi na Bw. Mkurugenzi wa shirika hilo, Bw. Salim Mwaking’inda ambaye hakuwepo mahakamani kutokana na kufiwa na mtoto wake.

Mbele ya Hakimu Bw. Faisal Kahamba, wakiliwa Serikali kutoka Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Bi. Mariagoleti Richard, alidai shauri hilo limefikishwa mahakamani hapo kwa ajili ya kutajwa na kupangiwa tarehe ya kuwasomea  washtakiwa maelezo ya awali.

Wakili upande wa utetezi Bw. George Mdimo, alitoa taarifa za kutokuwepo kwa mshtakiwa huyo na kudai kuwa, alileta barua mahakamani hapo ya kutoa taarifa ya msiba uliompata.

Hata hivyo, Bi. Richard alidai taarifa hiyo haikumfikia tangu awali ambapo wadhamini wa mshtakiwa huyo, wangepeswa kuwepo mahakamani kutoa taarifa badala ya kuandika barua.

Kesi hiyo imeahirishwa hadi Julai 19 mwaka huu, itakapoletwa kwa ajili ya kutajwa na kupangiwa terehe ya washtakiwa kusomewa maelezo ya awali. Katika kesi hiyo, Bw. Simba, alikuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya UDA.

No comments:

Post a Comment