16 May 2012

Ubabe sio suluhu ya kumaliza mgomo



Na Grace Ndossa

JUZI mgambo wa Manispaa ya Ilala walimzuia  Mkurugenzi wa Manispaa hiyo Bw. Gabriel Fuime kuingia ofisini na wafanyakazi wake wakishinikiza kusikilizwa madai yao.

Askari hao waligoma kufanya kazi  kwa wiki tatu ili kushinikiza manispaa hiyo  kuwalipa madai yao ya msingi ya muda mrefu ndipo waweze kuingia katika mkataba  mpya.


Wanamgambo hao walieleza  kuwa, wameitumikia  Manispaa hiyo kwa zaidi ya miaka  kumi bila kupewa ajira za kudumu na kubaki kuwatumia  kwa faida zao binafsi.

Walieleza kuwa  walipoanza kazi katika manispaa hiyo walianza kwa mikataba ya muda mfupi walipoamaliza mikataba hiyo waliingia mkataba mwingine mipya ambayo mpaka leo hawajapewa stahiki zao.

Madai mengine ni marekebisho  kiwango cha shilingi elfu 4000 kwa siku wanachopewa ambacho ni kidopgo hivyo kuhitaji viwango vinavyolingana na maisha ya sasa.

Walieleza kuwa wamechoshwa  kugeuzwa vibarua wa muda mrefu na madai yao ya msingi yanashindwa kutekelezwa kwani wanahitaji mikataba inayofuata sheria za kazi ambapo mwaka jana waliahidiwa kuongezewa mishahara lakini hadi leo hakuna kilichofanyika.

Cha Kushangaza  walikaa muda wa wiki moja  kushinikiza uongozi wa  Manispaa hiyo kuwapa malimbikizo na kuboresha mikataba yao kutokana na kazi ngumu wanazozifanya na vikwazo wanavyokumbana navyo kila siku.

Askari hao hufanya  kazi mbali mbali za Manispaa na kuhakikisha hakuna wafanyabiashara wanaouza bidhaa katika sehemu zisizo rasmi na kuondoa wamachinga katika maeneo yasiyoruhusiwa.

Kitendo cha Manispaa hiyo kukaa kimya kwa muda mrefu bila kutatua matatizo ya askari hao ni cha dharau kwani inaonesha wazi kuwa wanawatumiwa bila malipo na kupoteza nguvu zao.

Pia  kitendo cha kutolewa kauli ambazo siyo nzuri kwa wafanyakazi hao sio cha kiungwana kwani viongozi hao wanatakiwa kujua kwamba Cheo ni dhamana na usipokitumia vizuri kinaweza kukuletea matatizo.

Nionavyo kitendo cha kuchelewa kusikilizwa na kujibiwa kuwa wao walikuwa vibarua tu na hawakuwa na mikataba ya ajira katika kufanya kazi kwani   wana askari wa kutosha kufanya kazi walizokuwa wanazifanya hakikuwa cha kiungwana.

Kama kweli walikuwa na askari wa kutosha kufanya hizo kazi kwanini wawatafute mgambo hao kwenda kuwafanyia kazi na wengine wamepoteza hata meno yao kwa kupambana na wahalifu katika jiji hilo na bila hata kuwapatia fedha za matibabu.

Pia nashindwa kuelewa kwamba hata Mkurugezi wa Manispaa hiyo alipotafutwa kuzungumzia suala hilo alijibu na kueleza kwamba  walikuwa ni vibarua tu kwani hataka kama mtu akiwa kibarua si anatakiwa  kupewa kilicho chake na kuelezwa kwamba kwa sasa hatutahitaji tena vibarua hadi hapo kazi zitajitokeza.

Manispaa hiyo kwa dharau  bila kuwaita na kuwaeleza wanatoa tangazo kwenye ubao wa matangazo wanaeleza kuwa askari hao sii wanamgambo tena wa manispaa hiyo hicho siyo kitendo cha uungwana lazima wawe na utu na hofu ya mungu katika  maamuzi yao.

Kauli hizo zilizaa mgogoro uliodumu kwa wiki tatu wakati wangetumia muda mfupi kumaliza mgogoro huo.

Pia walipaswa kuwapa haki zao hata kama walishindwa kuwalipa wale waliopata  adha katika sehemu ya kazi kwani wengine hawana meno kabisa kutokana na vuta nikuvute katika sehemu zao za kazi.

Viongozi wakumbuke kuwa viapo walivyoapa katika kufanya kazi wafanye kwa uaminifu kwani kabla ya kupata kazi hizo unawakuta wakijinadi kwa wananchi kwamba watatatua matataizo ya wananchi yanayowakabili lakini wakishapata madaraka wanasahau kabisa.

Ikumbuke kuwa hizo nafasi walizonazo wanatakiwa wawe wakarimu na kuwa na lugha nzuri kwa wafanyakazi ili  hata kama huna fedha za kumlipa leo wala kesho aweze kuwa na matumaini na siyo kutoa maneno ya kashfa .

Viongozi wa namna hiyo ni wale ambao hawatakiwi katika jamii kwani wanashindwa kutumia mamlaka waliyonayo kuzungumza na wafanyakazi kero zinazowakabili na kuzipatia ufumbuzi, wakae wakijua kwamba kutumia ubabe siyo suluhu ya matatizo.

Hata hivyo viongozi wengi wanasubiri matatizo yakishakuwa makubwa ndiyo wanakaa chini na kulitafutia ufumbuzi badala ya  kutatua pale mwanzoni linapotokea.

Hawa ndiyo viongozi wetu wanaotuongoza kwani tatizo lishakuwa kubwa ndiyo wanakumbuka kuwa kuna kukaa chini  katika meza ya mazungumzo na kufikia muafaka, kweli tukienda hivyo hatuwezi kufika sehemu yoyote.

Hata kwa msingi wa kufikia utawala  bora  hatutafika kwani  serikali inapompa mtu dhamana ya kuongoza katika eneo lolote anajua uwezo wa  kuongoza anao lakini  anapofika pale anajua akitumia lugha ya kibabe ndiyo atafanikiwa.

Kiongozi yoyote ukipewa dhamana ya kuongoza lazima uwe  na lugha laini ya kuongea na wafanyakazi na kuhakikisha kuwa mahusinano  na mawasiliano mazuri  katika sehemu ya kazi ili wafanyakazi waliopo waweze kuwajibika  ipasavyo.

Pia anapaswa kutambua kuwa kiongozi mzuri ni yule anayekaa na wafanyakazi na kuzungumza nao, kushaurina na wafanyakazi na siyo kuchukua maamuzi yake mwenyewe kama avyoelewa, pia kuondoa  nafasi iliyoachwa wazi kati ya wafanyakazi na viongozi wao pamoja na  kutumua elimu yake aliyoanayo  kuhamasisha wafanyakazi wawajibike ipasavyo.

No comments:

Post a Comment