01 February 2012

RUBADA:Miundombinu ya Mto Kilombero iboreshwe

Na Mwandishi Wetu,
Morogoro

UBORA  wa miundombinu katika Mto Kilombero imeelezwa kuwa ni suala muhimu kufanikisha mkakati wa Kilimo Kwanza na uendelezaji wa ukuaji wa kilimo katika Ukanda wa Kusini mwa Tanzania (SAGCOT) mkoani Morogoro.


Hayo yalibainishwa na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Uendelezaji wa Bonde la Mto Rufiji (RUBADA), Bw. Aloyce Masanja wilayani Kilombero mkoani Morogoro wakati akizungumzia tatizo la miundombinu katika kivuko cha Mto Kilombero hivi karibuni.


Alisema mkakati wa 'Kilimo Kwanza' utafanikiwa kama  juhudi zitazingatiwa za kuwepo  kivuko chenye uhakika katika Mto Kilombero kutokana na kivuko kilichopo  kutokuwa na uwezo mkubwa wa kupitisha mizigo kutoka upande mmoja kwenda mwingine.



“Kivuko hiki kimekuwa ni kikwazo kikubwa sana kwa wananchi wa maeneo haya na hasa katika bonde la mto kilombero, kwa hiyo kinachohitajika ni kuweka mkakati wa dhati wa kuhakikisha kuwa kunakuwa na mpango wa muda mrefu wa kuondokana na tatizo lililopo sasa la kivuko,” alisema Masanja.



Aliongeza kuwa ili kuendana na dhana ya Kilimo Kwanza ni lazima pawepo na njia mbadala ya kuondoa shida iliyopo kwa sasa, na kusisitiza kuwa njia pekee ya kuondokana na adha iliyopo ni kuwa na daraja katika eneo hilo.



“Kwa sasa mamlaka imejikita katika kupanua maeneo kwa ajili ya uwekezaji, hivyo ni vema daraja likaboreshwa  ili kuweza kuwavutia wawekezaji wengi kuja kuwekeza katika sekta ya kilimo katika bonde la mto kilombero,” alisema Masanja.



Kwa sasa wawekezaji ambao tayari wamejitokeza ni wale wanaolima mpunga katika shamba la Mngeta huku mafanikio yakionekana kuwa mazuri kutokana na wananchi wa maeneo jirani kufaidika na uwekezaji mkubwa uliopo katika shamba la Mngeta.


Katika kutekeleza azma hiyo ya kuwa na kivuko cha uhakika ama mpango wa muda mrefu wa  ujenzi wa daraja ili kuwavutia wawekezaji tayari RUBADA  walikutana na wadau mbalimbali katika sekta ya kilimo ili kuona uwezekano wa kutatua tatizo hilo.


“Tulikubaliana kuwa tushirikiane pamoja na watoa maamuzi ili tuweze kujenga daraja katika eneo hili na kutekeleza mkakati mzima wa kilimo kwanza,” alisema Masanja.


Alisema maazimio mengine katika kikao hicho ni uwezekano wa taasisi za serikali kushirikiana na sekta binafsi kuona uwezekano wa kuleta kivuko kipya au kujenga daraja katika eneo hili la Mto Kilombero.




No comments:

Post a Comment