13 January 2012

Mafunzo ya kujiepusha na madawa ya kulevya

Na Zena Mohamed

WANAFUNZI wa darasa la saba katika Shule ya Msingi Chang'ombe Wilaya temeke jijini Dar es Salaam wamepewa elimu jinsi ya  kujiepusha na matumizi ya dawa za kulevya na  mtalaam wa  somo la stadi za maisha Bw.Yuki Koga  kutoka nchini Japan.

Bw.Yuki alitoa elimu hiyo jana shuleni hapo baada ya wanafunzi hao kutembelewa na mwanamuziki  kutoka Shirika la Maendeleo la Japan (JICA) Bw. Sadao Watanabe.

Alisema lengo la kuwafundisha  somo hilo wanafunzi hao ni kuwajengea mazingira ya  kujitambua iliwajue wanachokifanya na kujua kitu  kibaya na kizuri kwao katika kufanya maamuzi yao.

"Nimeona katika Wilaya ya Temeke Vijana wengi wanatumia madawa ya  kulevya ndio maana nikaamua kuwaelimisha wanafunzi wa darasa la saba ili wajue madhara yake kwasababu ndio wanatoka kwenye utoto wanakwenda kwenye ujana," alisema Bw. Yuki.

Bw. Yuki aliigiza igizo fupi ilikuweka msisitizo zaidi kwakutumia  vitendo na kuwafanya wanafunzi hao kuelewa zaidi athari za dawa hizo.

Alitaja baadhi ya madhara yanayoweza kujitokeza baada ya matumizi ya dawa hizo kuwa ni kushawishika na kuweza kufanya ngono isiyo salama na kusababisha kupata magonjwa kama Ukimwi na Kisonono.

Pia alisema atafundisha somo hilo kwa muda wa mwaka mmoja katika Shule zote za Msingi Wilaya ya Temeke.

No comments:

Post a Comment