20 January 2012

Katiba Mpya iwanufaishe wananchi katika ardhi, mazingira

Na Peter Mwenda

ASILIMIA 70 ya Watanzania wanategemea ardhi, mazingira na maliasili ili wanufaike hivyo Katiba Mpya
ni vyema ikatamka wazi jinsi wananchi watakavyonufaika.
Jaji mstaafu Mark Bomani, aliyasema hayo Dar es Salaam jana katika mjadala wa Jukwaa la Katiba.
Alisema upo umuhimu mkubwa wa Katiba Mpya kueleza wazi jinsi Watanzania watakavyonufaika na ardhi, mazingira na rasilimali tofauti na ilivyo sasa.
Aliongeza kuwa, suala la mazingira na maliasili halipaswi kuachwa ili kuondoa tatizo la uharibifu uliopo kwani katiba ya sasa haijaweka wazi juu ya suala hilo.
Jaji Bomani alisema, katiba sio kitabu kitakatifu bali inaweza kubadilishwa kulingana na wakati husika.
 Katiba ya sasa haina vifungu rasmi vinavyozungumzia mazingira na rasilimali asilia kwa kina, mambo hayo mawili ni muhimu kuelezwa kiundani badala ya suala hili kushughulikiwa na bunge.
 Kwa mpano, Katiba Mpya nchini Kenya, ina zungumzia mazingira na maliasili, hili ni jambo la kuiga, si lazima Watanzania wote zaidi ya milioni 44 wachangie mawazo yao, vikundi mbalimbali maoni yao kwa tume ambayo itaundwa na rais,¡± alisema.
Alisema wakati akiwa Mwenyekiti wa Tume ya Kupitia Sekta ya Madini miaka mitatu iliyopita, aliwahi kusema upo uwezekano mkubwa wa ardhi ya Tanzanmia kubaki mashimo kutokana na uchimbaji madini unaofanywa na wageni.
Aliongeza kuwa, bila kuwa na usimamizi mzuri katika mazingira na rasilimali kila mtu atafanya jambo analoona linafaa hivyo hali hiyo itasababisha uharibifu mkubwa wa mazingira.
 Anayepewa leseni ya kuchimba madini, apewe na masharti pamoja na kulipa fidia wananchi ambayo itawanufaisha wakazi wa eneo husika,¡± alisema Jaji Bomani.
Mwenyekiti wa jukwaa hilo, Bw. Deus Kibamba, alisema semina hiyo imelenga kujadili mambo yanayoweza kujitokeza katika mchakato wa kuandika Katiba Mpya.
Semina hiyo iliyoandaliwa na Jukwaa la Katiba Tanzania kwa kushirikiana na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Idara ya Geografia.

No comments:

Post a Comment