25 January 2012

Kampuni zashauriwa kujiunga na 'Bacordes'

Na  Agnes Mwaijega

KAMPUNI na wazalishaji wa bidhaa mbalimbali nchini wametakiwa kujiunga na mfumo mpya wa kuweka alama za utambulisho za mistari 'Bacordes' katika bidhaa zao ili kuongeza kiwango cha manunuzi ya bidhaa hizo.
Akizungumza Dar es Salaam jana katika Mkutano Mkuu wa Taasisi ya GS1 (TZ) National Limited,  Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda na Biasahara Bi.Joyce Mapunjo alisema kwa muda mrefu  bidhaa zinazotengenezwa nchini zimekuwa zikitumia 'Bacordes' za nchi zingine hivyo kuifanya nchini yetu kushinwa kujulikana.

Alisema mfumo huo ni muhimu na utasaidia uchumi wa nchi kukua na bidhaa zinazotengenezwa nchini kuweza kutambulika duniani kote.

Alisema mfumo huo pia utasaidia kupunguza na kudhibiti wizi wa bidhaa unaofanywa na watu mbalimbali hivi sasa.

"Mfumo huu umewezesha nchi nyingi zilizoendelea kuwa na mafanikio makubwa kiuchumi na kuwaongezea kipato wafanyabiasahara," alisema.

Aliongeza kuwa mfumo huo pia utasaidia kupunguza gharama za uendeshaji wa biashara nchini na kuwajengea mazingira bora wafanyabiashara na wazalishaji wa bidhaa mbalimbali.

Hata hivyo alitoa mwito kwa taasisi hiyo kuhakikisha inahamasisha uzalishaji wa bidhaa bora na zenye tija kwa maendeleo ya taifa na wafanyabiashara kwa ujumla.

Alisisitiza kuwa mfumo huo uendelee kufanyiwa utafiti zaidi ili uweze kuleta mafanikio makubwa katika sekta ya uchumi nchini.

No comments:

Post a Comment