29 December 2011

NCCR: Kafulila amejipalia mkaa

*Dkt. Mvungi: Washauri wake wanamdanganya
*Asema Mahakama haijatengua azimio la kikao
*Kafulila: Sina cha kusema, naheshimu uamuzi


Na Peter Mwenda

CHAMA cha NCCR-Mageuzi, kimesema mbunge wake wa Kigoma Kusini Bw. David Kafulila, ambaye alivuliwa uanachama kutokana na
utovu wa nidhamu, amejipalia mkaa baada ya kupinga uamuzi huo katika Mahakama Kuu, Kanda ya Dar es Salaam.

Tamko la chama hicho limetokana na uamuzi uliotolewa juzi na Mahakama hiyo kusimamisha utekelezwaji wa azimio la kikao cha Halmashauri Kuu ya chama hicho kumvua uanachama.

Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Katibu wa Idara ya Katiba na Sheria wa chama hicho, Dkt. Sengondo Mvungi, alisema washauri wa Bw. Kafulila wanamdanganya kwa hatua anazochukua na kujichimbia kaburi.

Alisema amri iliyotolewa na Jaji Alise Chinguwile wa Mahakama hiyo ni kuzuia utekelezwaji wa azimio la kikao cha dharura cha Halmashauri Kuu ambacho kilikaa Desemba 17 mwaka huu, hadi kesi ya msingi itakapokwisha lakini si kutengua azimio la kikao.

“Magazeti mengi yaliyotoka leo (jana), sio Majira, yameandika vitu tofauti na amri ya Mahakama Kuu, nasema kwa mara ya kwanza waandishi wamechakachua amri ya mahakama kwa kusema uwongo,” alisema Dkt. Mvungi.

Aliongeza kuwa, amri ya Mahakama imeombwa na Bw. Kafulila akiitaka NCCR-Mageuzi na Mwenyekiti wake wa Taifa, Bw. James Mbatia, wazuiwe kuchukua hatua zaidi dhidi yake sambamba na kusitisha vikao vya kujadili suala hilo.

“Bw. Kafulila aliandika barua Desemba 19 mwaaka huu ya kupinga kuvuliwa uanachama na kuorodhesha kasoro ambazo chama kingekaa kuzijadili lakini kwa sababu Mahakama imezuia, hakuna kitakachofanyika kwa ajili yake.

“Kimsingi amejiua mwenyewe lakini baadhi ya vyombo vya habari vinamshangilia, huyu ni kijana wetu lakini hataki kufuata tunayomtaka afafuate,” alisema Dkt. Mvungi.

Aliongeza kuwa, Bw. Kafulila alipaswa kufuatilia maombi ya barua yake ya kuomba kuitishwa kikao cha Halmashauri Kuu ili aombe msamaha na kusubiri majibu ya chama hicho kwa Msajili wa Vyama vya siasa Bw. John Tendwa, aliyetaka ufafanuzi wa mtafaruku huo badala ya kwenda kujishindilia msumari mahakamani.

Alisema nchi za Rwanda na Burundi, ziliingia katika mauaji ya Kimbari baada ya waandishi kuchangia hisia hasi na kusababisha mauaji.

“NCCR-Mageuzi haijachukua uamuzi huu kwa kicheko, hakuna sababu ya kushangilia, sisi tumeumia hivyo hakuna sababu ya kuandika habari za uwongo ambazo hazipo katika amri ya Mahakama,” alisema.

Akizungumza na Majira kwa njia ya simu jana, Bw. Kafulila alisema hayupo tayari kumjibu Dkt. Mvungi kwa sababu suala hilo lipo mahakamani kwani yeye binafsi, anaheshimu maamuzi ya mahakama.

“Kama Dkt. Mvungi anaweza kuzungumzia mambo ambayo yapo mahakamani, yeye aendelee, mimi sipo tayari kwa sababu naiheshimu Mahakama,” alisema Bw. Kafulila.

Bw. Kafulila na wenzake nane, walipeleka shauri namba 218 katika mahakama hiyo kuzuia uamuzi wa chama hicho kumvua uanachama na kusimamisha vikao vyenye lengo la kujadili suala lake.

6 comments:

  1. DR. MVUNGI:-

    Alisema nchi za Rwanda na Burundi, ziliingia katika mauaji ya Kimbari baada ya waandishi kuchangia hisia hasi na kusababisha mauaji.

    “NCCR-Mageuzi haijachukua uamuzi huu kwa kicheko, hakuna sababu ya kushangilia, sisi tumeumia hivyo hakuna sababu ya kuandika habari za uwongo ambazo hazipo katika amri ya Mahakama,”

    HAYA MAGAZETI KAMA MWANANCHI NA TANZANIA DAIMA WAKURUGENZI WAKE NA WAHARIRI WANALIPWA PESA NYINGI KUCHAFUA NCHI NA HABARI. WATAIANGAMIZA NCHI. BORA NA WEWE UMELIONA. KWENYE GAZETI LA MWANANCHI UKIANDIKA HABARI YA KUIPONDA CHADEMA HAYAANDIKWI WAO KAZI YAO KUJAZA MAMBO YA KUPONDA VYAMA VINGINE TU. ANGALAU HAPA MAJIRA TUNAJITANUA MAANA UKIMALIZA INAANDIKA LAKINI MWANANCHI ADMINISTRATOR ANACHAKACHUA KWANZA AKIONA MABWANA ZAKE WANAPONDWA HAANDIKI

    ReplyDelete
  2. Hivi kwa nini usuluhishi wa matatizo ktk vyama usimalizikie kwenye vikao halali vya VYAMA??

    Mbona kuna vyama wanagombana lakini inafikia muda wale wanaosababisha ugomvi hujulikana wazi baada ya kufanya vikao?

    TUJADILI MATATIZO YETU NDANI YA VYAMA VYETU KWA KUWAITA WANAOTUVURUGA TUWASIKILIZA KABLA YA MAAMUZI KICHAMA.
    .

    ReplyDelete
  3. wanachokionyesha watanzania kuhusu uamuzi wa wana NCCR mageuzi ni mazoea ya kulindana.huyu kijana alipewa nafasi ya kujitetea na hajalalamika kwamba utaratibu wa kumfukuza ulikiuka katiba ya chama isipokuwa mashabiki wa chama tawala wao wanasema kwa kuwa ni mbunge angelionywa tu kwani kumfukuza mbunge ni ghalama sioni mantiki juu ya hili;chama kina katiba na ile katiba haibagui hatua za kuchukua kwa mwanachama wa kawaida na wabunge na kama imefuatwa sioni tatizo;tukianza kutumia mazoea ya watawala ya kuwa na watu walio juu ya sheria nafikili tutaharibu nchi;wananchi tuwe makini na tusishabikie kila kitu kinachosemwa kuna vingine ni vya hovyo.ninajiuliza wanaozungumuzia kuhusu ghalama za uchaguzi mdogo kwani wameliona leo? siku zote ghalama hizo zipo lakini huwa hawasemi kwa nini leo, haya ndio mambo ambayo yanapaswa kuangaliwa katika katiba mpya lakini nayo hawaitaki sasa wanataka nini? liliwahi kutolewa pendekezo la uwakilishi wa uwiano ikaonekana chama tawala hakikufurahi lakini ungelipunguza haya maghalama bahati mbaya wanaolalama sasa walibaki kimya;ikaja mgombea binafsi akakataliwa pia wanaolalama sasa walibaki kimya leo hii wanachonga midomo.vyama visiogope kuwapiga chini wanaokose ;kubebana wawaachie CCM WENYE AGENDA MOJA KILA SIKU KWA MIAKA NENDA RUDI.

    ReplyDelete
  4. hapo mmeongea mwananchi sio gazeti la uzalendo wala halina faida kwa mtanzani, nimeandika coment hivi asubuhi ya kwamba hata mgogoro wa cuf wanaripoti mambo ya kumpendelea hamad rashid tu na habari za uongo ndio kazi yao badala ya kuandika habari kwa kuweka haki katika pande zote wao wanabezi upande ambao wamelipwa posho kuchafua vyama vingine na hiyo coment yangu aikutolewa lakini kuna coment mtu kandika cuf ccm b imewekwa haraka sana kazi yao ni unafiki na uchochezi tu bora hapa majira unapata nafasi ya kutoa maoni kwa uwazi na haki cc kama watz hatutaki upendeleo kwa media na kutoa habari za upendeleo na uchochezi. mungu ibariki tz amin

    ReplyDelete
  5. hakuna gazeti linaloandika ukweli. Ukweli huwa ukweli baada ya mawazo uliyonayo wewe kufikiwa, huo ndio ukweli kwa mwanadamu. Mawazo yako yakitofautiana na unachokijua wewe..aah limeandika uzushi. Acheni wahariri wafanye kazi yao.

    ReplyDelete
  6. Sote tuna mitizamo yetu waacheni wana habari wafanye kazi zao.Vyombo vya habari vikiminywa hakuna demokrasia lakini uzalendo kwanza.

    ReplyDelete