27 September 2011

CUF yatolea uvivu CCM

Na Peter Mwenda, Igunga

CHAMA cha Wananchi (CUF) kimeng'ara katika mdahalo wa vyama vyenye nafasi kubwa ya kutwaa kiti cha ubunge wa Jimbo la Igunga baada ya Naibu Katibu Mkuu wake
, Bw. Julius Mtatiro kukitolea uvivu CCM kuwa ndicho kinasababisha vurugu na kuandaa makundi ya vijana nje ya  Igunga.

Bw. Mtatiro aliyepata nafasi ya mwisho kutoa nasaha zake upande wa viongozi wa vyama vilivyoshiriki mdahalo huo, alisema CCM imeshindwa kuwasaidia wananchi wa Igunga kwa miaka 50 tangu uhuru, hivyo kimezeeka, kinatakiwa kipishe maendeleo yaletwe na wapinzani hasa mgombea wa chama chake, Bw. Leopold Mahona.

Akishangiliwa na wafuasi wa CUF, Bw. Mtatiro alisema CCM imeweka makundi ya vijana lakini haijulikani wamekwekwa katika makambi kwa ajili ya sababu gani.

Bw. Mtatiro aliyejibu kauli ya Katibu wa Fedha na Mipango wa CCM, Bw. Mwingulu Nchemba aliyewataka Wanaiunga wachague CCM kwani ndicho chenye kuhubiri amani na upendo, alisema wananchi wa Igunga wasijidanganye kuchagua kiongozi mwenye jina kubwa, mwisho wa siku watabaki wakijuta.

Kabla ya Bw. Mtatiro kumaliza mdahalo kwa kauli hiyo, Naibu Katibu Mkuu CHADEMA, Bw. Zitto Kabwe alisema wananchi wa Igunga hawako tayari kuendelea kusikia nani kavuliwa hijabu wala malumbano ya visasi, bali wanataka mbunge wa kubadilisha maisha yao.

Katika mdahalo huo, wagombea wa ubunge kupitia CUF, Bw. Mahona na yule wa CHADEMA Bw. Joseph Kashindye walimweka kati mgombea wa CCM, Bw. Dalaly Kafumu kuwa ameshindwa kusaidia wachimbaji wadogo wa madini wa Igunga akiwa na wadhifa wa Kamishna wa Madinin katika Wizara ya Nishati na Madini.

Awali, Bw. Mahona akieleza sera zake katika mdahalo huo alisema akichaguliwa atatumia rasilimali zilizopo kusaidia vijana na akinamama kupata ajira.

Naye Bw. Kashindye alisema akichaguliwa kuwa mbunge wa jimbo hilo atahakikisha anasimamia na kudhibiti mianya yote ya rushwa na matumizi mabaya ya fedha za umma.

Hata hivyo, mgombea huyo alikumbana na changamoto ya kurushiwa tuhuma za ubadhilifu katika moja ya vituo vya elimu alipokuwa mwalimu katika Kata ya Simbo.

Akijibu tuhuma hizo Bw. Kashindye alibainisha kuwa tuhuma hizo si za kweli kwani yeye hakuhusika na madai hayo badala yake yeye alisimamia utendaji kazi na kusababisha kupandishwa cheo mara baada ya kuhamishwa.

Wakati huo huo, ibada ya kuombea uchaguzi mdogo wa Ubunge Jimbo la Igunga ilifanyika mjini hapa na kushirikisha makanisa tisa ya kikristo.

Katika ibada hiyo viongozi wa serikali walitakiwa kujiepusha na kauli zenye kuchochea vurugu katika jimbo la Igunga.

Mwenyekiti wa Umoja wa Makanisa hayo, Padri Joseph Maziku kutoka Kanisa Katoliki alisema umoja huo haupo tayari kuona wananchi wa Igunga wakimwaga damu kwa ajili ya tamaa za viongozi wanaotaka madaraka kwa nguvu.

Madhehebu yaliyohudhuria ni pamoja na Kanisa la Babtist, Efatha, KKKT, Moravian, Anglikani, Kanisa Katoliki, TAG, EAGT, EPCT na kila kanisa lililoongoza maombi.

2 comments:

  1. Ni kweli kabisa vurugu, ubabe na vitendo viovu kama uzinzi vinafanywa na CCM kwa kujidai wao ni chama tawala. lakini siku zinavyozidi ukweli utajulikana na wananchi wa TZ watajua pumba zipi na mchele upi. Siku Rage aliposimama jukwaani akiwa na bastola hakufanywa lolote na Polisi walikuwepo. Ninaamini kabisa angekuwa ni mpinzani angeshughulikiwa

    ReplyDelete
  2. POLENI WATANZANIA KWANI MPAKA DAKIKA HII HAMJAJUA KUWA ADUWI YENU NICHA TAWALA CCM AMBACHO KIMEWAWEKA PABAYA KIELIMU, KIUCHUMI, KIAFYA NA KUTEKETEZA MALI YA UMMA KWA KUWAPA WAGENI LASRIMALI NA WANANCHI KUBAKI MIKONO MITUPU. MTAENDELEA KUDANGANYWA KUWA MTAJI WA MASKINI NI NGUVU ZAKE MWENYEWE WAKATI MTAJI WA WABUNGE WA CCM NI NGUVU ZA UMMA. WATANZANIA MTAKUWA NA AKILI PALE MTAKAPO KIONDOA CHAMA TAWALA MADARAKANI ILI WENGINE WALETE MABADILIKO. ACHENI KUPIGA MAKELELE KWANI MTATIZO MNAYA FUGA WENYEWE KWA KUPOKEA TUKANGA NA TUVITENGE ILI MUWAOIGIE KURA NA KISHA WAENDELEE KUNEEMEKA. WATANZANIA ONDOWENI CCM MADARAKANI MUTAONJA URAIA WA KWELI.

    ReplyDelete