03 May 2011

Aliyenyonga watoto adai kuambiwa hawakuwa wake

Na Mashaka Mhando, Tanga

MWANAUME anayetuhumiwa kuwaua watoto wake wawili katika mji mdogo wa Misima wilayani Handeni, Mashaka Athumani (45) amekamatwa na polisi akiwa
mashambani na kudai anadhani amelogwa kufanya kitendo hicho, baada ya kauli ya mkewe kwamba watoto hao hawakuwa wake.

Ofisa Mtendaji wa Kata ya Misima, Bw. Zahoro Semdoe alisema mtuhumiwa huyo baada ya kukamatwa katika kitongoji cha Masampata kilichopo kijiji cha Malezi kata ya Chanika akiwa amejificha shambani kwa mkwewe aliyeoa bintiye, alidai kuwa tangu kuanza kwa ujenzi wa barabara ya lami inayojengwa na kampuni ya Kichina ya Sinohyodro, mahusiano yake na mkewe hayapo vizuri kwa madai kwamba anahisi yupo mkandarasi, mwenye mahusiano na mkewe.

Alisema hali hiyo imekuwa ikiendelea na wakati mwingine mkewe huyo alikuwa
akimweleza kwamba watoto aliozaa naye hawakuwa wake, hivyo akamtaka aondoke kwenye nyumba waliyokuwa wakiishia ambayo ni ya urithi wa mkewe, hatua ambayo ilimfanya akose amani mara kwa mara anapofika nyumbani hapo.

"Mimi nikiwa kama mlinzi wa amani wa Kata ya Misima alipokamatwa na kuhojiwa, kwanza alielezea kujutia tukio lile kwa kudai huenda amelongwa kufanya hivyo, lakini pia alidai ametakiwa kuondoka katika ile nyumba atafute pa kwenda kuishi kokote na amwache huru kwa vile watoto aliozaa naye pia hawakuwa wake," alisema ofisa huyo.

Akielezea zaidi namna ya mtuhumiwa huyo alivyokamatwa usiku wa kuamkia juzi, Bw. Semdoe alisema alikutwa amelala katika shamba la mahindi la mkwewe usiku, ambapo alikuwa kifanyiwa taratibu za kutoroka kwenda mbali ili kuwakimbia polisi.

Alisema kuwa taarifa za kukamatwa mtuhumiwa zimekuja baada ya awali kusikia kwamba mtuhumiwa huyo amejinyonga mwenye na ameonekana porini akiwa amejitundika, lakini baadaye wakapata taarifa yupo katika kitongoji hicho na alikuwa akifanyiwa utaratibu wa kutoroshwa.

Mtuhumiwa huyo anadai kuwa anazidi kuchanganyikiwa akifikiria unyama aliowafanyia watoto wake hao kwa kuwanyonga hadi kufa.

Kaimu Kamanda wa Polisi mkoani Tanga, Bw. Jafari Mohamedi amekiri mtuhumiwa huyo kukamatwa na alisema kuwa wanafanya uchunguzi kuhusiana na tukio hilo kabla ya kumfikisha mahakamani wiki hii kujibu tuhuma zinazomkabili.

Kamanda Bw. Mohamedi aliwapongeza wananchi hao pamoja na viongozi waliotoa
ushirikiano hadi kufanikisha kukamatwa kwa mtuhumiwa huyo anayedaiwa kuwaua watoto wake Amina Mashaka (7) ambaye alikuwa ni mwanafunzi wa darasa la kwanza Shule ya Msingi Misima na Masefu Mashaka
mwenye umri wa miaka miwili na nusu.

1 comment:

  1. apewe adhabu kubwa kama aliyowapa watoto wake.

    ReplyDelete