15 March 2011

Muarobaini wa mgawo wa umeme watajwa

Na Tumaini Makene

VYANZO vya umeme vya Kiwira, Ngaka na Mchuchuma pekee, ambavyo kwa ujumla vinazalisha megawati 1,500 kwa nchi zima, vinaweza kuiokoa nchi na tatizo la umeme uliopo kwa sasa nchini kwa zaidi ya miaka 100 ijayo, kutengeneza ajira na kukuza uchumi nchini.

Pia imeshauriwa kuwa ili Shirika la Umeme nchini litumie rasrimali zake vizuri kutoa umeme wa uhakika kwa wananchi, pia kuokoa fedha za bajeti ya serikali kutumika kuzalisha umeme, shirika hilo sasa linapaswa kuacha kuzalisha badala yake lijikite katika kujenga miundo mbinu ya kugawa na kusafirisha nishati hiyo,

Hayo yalisemwa jana Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Hesabu ya Mashirika ya Umma, Bw. Zitto Kabwe kuwa kamati yake, inao mpango wa kushauri shirika hilo lisijihusishe na uzalishaji, badala yake 'uwekezaji' huo ufanywe na mashirika mengine ya serikali au binafsi kama vile Shirika la Maendeleo ya Taifa (NDC), STAMICO, NSSF.

Akizungumza na waandishi wa habari jana katika semina ya wabunge kuhusu  usimamizi wa bajeti, Bw. Zitto alisema kuwa ni mzigo kwa TANESCO kuendelea kufanya kazi zote za kuzalisha, kusafirisha na kugawa umeme, kwani wakati mwingine zinahitaji uwekezaji wa fedha nyingi ambazo haziendani na uwezo wa shirika hilo.

Alisema kuwa pamoja na uwezekano wa nchi kupata umeme mwingi takribani megawati 1500, katika vyanzo vilivyoko kusini mwa Tanzania, bado hata ukipatikana leo hauwezi kutumika kwani TANESCO haina uwezo wa kuusafirisha kutokana na uchakavu wa miundombinu ya kuusafirisha.

Alisema kuwa vyanzo vya umeme vya Mchuchuma (mg 600),Ngaka (400) na Kiwira (500 mg) ambapo kwa pamoja vina uwezo wa kuzalisha megawati 1500 za nishati ya umeme ambayo inatosha kumaliza tatizo lililopo kwa takribani miaka 100 au 150 ijayo.

Alisema vyanzo vya nishati ya umeme vilivyopo katika Mikoa ya Nyanda za Juu Kusini inatosha kumaliza matatizo ya umeme iwapo serikali itaamua kuchukua hatua za haraka kuharakisha uzalishaji, ikiwemo utiaji wa mikataba kama vile ya NDC na Wachina na maombi ya NSSF kumiliki Kiwira.

"Mpaka sasa tunazalisha megawati 1034 tangu uhuru...miaka 50 yauhuru...lakini kwa kutumia vyanzo hivyo vitatu tu vya megawati 1500 tunaweza kuiokoa nchi hii na kutengeneza ajira na kukuza uchumi mbali ya kuzalisha umeme," alisema Bw. Zitto.

Bw. Zitto aliongeza kuwa kinachokwamisha mambo mengi nchini kushindwa kwenda kwa ajili ya kuinua maisha ya watu ni kukosekana kwa fikra za kujua kuwa nchi iko katika wakati mbaya, hivyo inahitajika kufanya maamuzi haraka, ambapo watu wote wanapaswa kufanya kazi kwa ajili ya nchi.

4 comments:

  1. UKWELI HIZI KAMATI ZINAFANYA KAZI NZURI YA KUKAGUA NA KUFAHAMU MAMBO MENGI TATIZO NI URASIMU ULIOPO KWA WATEKELEZAJI MAMBO KAMA HAYA HAYATAKI VIKAO VYA MUDA MREFU NI UAMUZI UCHUKULIWE WA HARAKA NA HUKU TARATIBU ZINGINE ZA KISHERIA ZINAFATA SERIKALI INATAKIWA IYAFANYIE KAZI HUU USHAURI MARA MOJA MFANO TOKEA KURUDISHA HUO MGODI WA KIWIRA MPK LEO HAKUNA KILICHOTEKELEZWA NA INAKUWA KAMA SEHEMU YA VIONGOZI KWENDA KUTAKA KUJIPATIA UMAARUFU KW MANENO MAZURI YASIYO NA VITENDO SERIKALI ITANGAZE UMEME NI JANGA LA TAIFA ILI HATUA ZA HARAKA KWA LAZIMA TENA SIO HIYARI KUYATELEZA HAYA

    ReplyDelete
  2. Huyu Kabwe amepata wapi takwimu ya kuwa 1,500MW zinatosha miaka 100 hadi 150 ijayo. Kiasi hicho cha umeme kitatosha miaka sana sana 10 na baada ya hapo umeme zaidi utahitajika. Chukua South Afrika, wao wanazalisha 42,000MW na bado hazitoshi. Juma hili wanazima kituo kimoja kinachozalisha 1,800MW kwa matengenezo.

    Nakubaliana na Kabwe kuwa TANESCO inabidi isaidiwe sana. Sijui kama ile sheria inayozuia mtu au shirika lingine lolote Tanzania kuzalisha umeme imepigwa panga.

    ReplyDelete
  3. Tungekwa na wanasiasa waliokomaa,na wenye upeo mkubwa kama Zitto,na mawazo yao yakafanyiwa kazi,tungepiga hatua..
    Hongera kijana.

    ReplyDelete
  4. Mchangiaji no,2 soma vizuri hajasema MW 1,500 zitatosha miaka 100,maana yake vyanzo vya umeme ktk migodi (mali ghafi) iliyoko ardhini inaweza kutufikisha miaka 100 hadi 150,muhimu mawazo ya hiyo kamati yao yakafanyiwa kazi Tanesco iwe kazi yake ni kuzidisha spidi ya kueneza nguzo za umeme na kukarabati zilizo mbovu wazalishaji wakawa wengine

    ReplyDelete