04 March 2011

Meli zatozwa faini kupunguza msongamano

Na Edmund Mihale

MAMLAKA ya Bandari (TPA) na Mamlaka ya Mapato nchini (TRA) zimeanza kuzitoza faini ya dola za Marekani 15,000 meli 11 za mafuta zilizotia nanga
katika Bandari ya Dar es Salam kwa kutokamilisha nyaraka muhimu zinaruhusu kupakuliwa mizigo katika bandari hiyo.

Akizungumuza na waandishi wa habari Dar es Saalam jana, Meneja wa Bandari hiyo, Bw. Casian Ngamilo alisema hatua ni moja ya sababu ya kuondoa msongamano ulipo katika bandari hiyo kwa sasa.

Alisema kutokana sera ya soko huria katika uingizaji mafuta, kumekuwa na ongezeko kubwa la kampuni za mafuta na kila moja huagiza mafuta kwa kadri inavyotaka kulingana na mtazamo wake katika bei ya soko.

Alisema pia matukio yanayoendelea sasa katika nchi za Kiarabu ni kichocheo cha kampuni nyingi za mafuta kujiweka sawa na uwezekano wa kupanda bei ya nisahati hiyo, hivyo kuagiza bidhaa hiyo zaidi.

"Hivi sasa meli nyingi za mafuta hupokea mafuta hayo kutoka katika meli kubwa ambazo haziwezi kufunga nanga katika Bandari ya Dar es Salaam .

"Meli hizo kubwa hutia nanga baharini karibu na mwambao wa Tanzania au mbali zaidi, na hivyo meli za mafuta huchukua muda mfupi kwenda na kurudi tena Dar es Salaam.

"Meli hizo hukaa nje ya bandari zikiwa bado hazijakamilisha mauzo au taratibu za mauzo na wanunuzi wa mafuta," alisema.

Akitoa mfano alisema kuwa meli ya Mt. Omega iliondoka Februari 1 mwaka huu na kurudi tena Dar es Salaam Februari 6, mwaka huu na tani 37,915 za mafuta ikiwa imetumia siku tano kwenda na kurudi.

Meli nyingine kuwa ni Mt High Nefel iliyoondoka Februari 16 mwaka huu na kurudi Dar es Salaam Februari 26 mwaka huu ikiwa na tani 34,860 za mafuta ilitumia siku nane.

"Hivyo utaona kuwa meli hizo 11 zilizoko nje ya bandari hii hazijakamilisha nyaraka na taratibu ikimwemo ya kulipa gharama za bandari na kusababisha msogamano," alisema.

Alisema msongamano huo unaonesha picha mbaya ya bandari, hivyo kuathiri soko la bandari kwa wenye meli mwengine wa nje ya nchi, kujenga mazingira hatarishi ya usalama wa bandari hususani katika suala la utekaji nyara wa meli unaoendelea sasa, na usalama wa nchi pia.

1 comment:

  1. Hiyo $ 15,00 wanayotozwa inalipwa na wananchi. Hali ni ile ile mzigo kwa mlalahoi.

    ReplyDelete