10 February 2011

Wanafunzi 1,700 wasimamishwa vyuo vikuu

*Wamo wa uandisi Mlimani, Teofilo Kisanji
*16 wapandishwa kizimbani mkoani Mbeya


Na Dunstan Bahai na Charles Mwakipesile

WANAFUNZI wote 1,200 wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kitengo cha
Uhandisi na Teknolojia (CoET) wamesimamishwa masomo kwa muda usiojulikana kutokana na kufanya vurugu chuoni hapo.

Vurugu hizo zilizoanza Ijumaa wiki iliyopita, zilihusisha baadhi ya wanafunzi hao kuwapiga wenzao na kuwazuia wasiingie darasani wakiushinikiza uongozi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kumrejesha mwanafunzi mwenzao wa mwaka wa nne, Jamson Babala aliyefukuzwa chuoni hapo kutokana na kukiuka taratibu na sheria za mitihani.

Akizungumza jana na waandishi wa habari, Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu, Profesa Rwekaza Mukandala, alisema hatua ya kuwasimamisha masomo wanafunzi hao imeamuliwa na vikao vya chuo vilivyokaa juzi na jana.

"Suala hilo lilijadiliwa katika kikao cha dharura cha Baraza la Chuo kilichofanyika Februari 8, 2011. Baraza liliagiza kwamba ikiwa vurugu zinazoendelea hazitasitishwa, masomo ya shahada za kwanza katika koleji ya Uhandisi na Teknolojia yasimamishwe na wanafunzi husika waondolewe chuo," alisema Profesa Mukandala.

Alisema kutokana na vurugu hizo zilizoanza Ijumaa wiki iliyopita, uongozi wa Chuo Kikuu umechukua uamuzi wa kutekeleza maelekezo hayo ya Baraza la Chuo ya kusimamisha masomo ya shahada za kwanza katika kitengo hicho cha Uhandisi na Teknolojia na kuwaondoa wanafunzi wote kuanzia wa mwaka wa kwanza hadi wa nne.

Akizungumzia sababu za vurugu hizo, Profesa Mukandala alisema Novemba 12, mwaka jana wakati wa mitihani ya marudio, mwanafunzi Babala wa mwaka wa tatu, alikutwa na msimamizi wa mitihani akiwa na karatasi, kktu ambacho ni kinyume na taratibu za mitihani.

Kwa mujibu wa Makamu Mkuu wa Chuo, mwanafunzi huyo baada ya kugundulika, aliamua kuitafuna na kuimeza karatasi hiyo lakini msimamizi alimtaka aandike na kutia saini tamko kwenye kitabu chake cha kujibia maswali kuthibitisha yaliyotokea, na alitii na kuendelea na mitihani yake.

Alisema Disemba 6, mwaka jana suala hilo lilifikishwa katika Kamati ya Masomo ya Shahada za Awali ambako mtahiniwa huyo alikiri kufanya kosa hilo, ingawa alisema karatasi hiyo haikuwa na maandishi yoyote.

"Pendekezo la kumwachisha masomo mwanafunzi huyo lilifikishwa katika Kikao cha Seneti Desemba 15, 2010 na kukubaliana na pendekezo hilo na hivyo kupitisha uamuzi wa kumuachisha masomo.  Baraza la Chuo Kikuu cha Dar es Salaam lilifahamishwa kuhusu uamuzi huo katika kikao chake kilichofanyika Januari 27, 2011 na likaridhia," alisema Profesa Mukandala.

Alisema kutokana na uamuzi huo wa Seneta, Januari 17 mwaka huu mwanafunzi huyo alimuandikia barua Makamu Mkuu wa Chuo akiomba radhi kwa yaliyotokea na kuomba kupunguziwa adhabu hiyo na hasa ikizingatiwa kuwa ni mwanafunzi wa mwaka wa nne huku matokeo yake ya mitihani iliyopita yakiwa ni ya kuridhisha.

"Kwa kuzingatia kanuni za mitihani na sheria nyingine, ombi hilo halikukubaliwa. Hivyo Jamson Babala akawa si mwanafunzi tena wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam," alisema.

Profesa alisema kuwa kutokana na uamuzi huo, wanafunzi wenzake wa Uhandisi na Teknolojia waliamua kufanya vurugu tangu Ijumaa wiki iliyopita, wakiwapiga wenzao na wengine kujeruhiwa vibaya na kwamba kesi zao ziko polisi kwa taratibu za kisheria.

Kuhusu masharti ya wanafunzi hao kurejea chuoni hapo, Profesa Mukandala alisema uchunguzi unaendelea kipindi watakachokuwa nje ya chuo na chuo kikijiridhisha kwa baadhi yao kutofanya vurugu, kitawarejesha.

Hali ya usalama chuoni hapo na katika hosteli ya Mabibo iliboreshwa na Profesa alisema kuwa hakukuwa na vurugu hadi jana.

Wasimamishwa Teofilo Kisanji

Chuo Kikuu cha Teofilo Kisanji mkoani hapa kimewasimamisha  wanachuo 508 wa mwaka wa tatu wanaosoma Historia kwa muda usiojulikana kwa kosa la kufanya vurugu na maandamano.

Miongoni mwao 16 wamepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Mkoa wa Mbeya kwa kosa hilo.

Akitangaza msimamo huo baada ya vikao vya uongozi wa chuo hicho kinachomilikiwa na Kanisa la Moravian Tanzania, Makamu Mkuu wa Chuo, Profesa Tuli Kasimoto alisema kuwa wanachuo hao waliamua kufanya vurugu kwa madai ya kutomtaka mwalimu wao somo hilo.

Alisema kuwa wanachuo hao wakichochewa na morali wa kisiasa  walianza vurugu hizo za kutaka mwalimu wa soimo la Historia aondolewa tangu January 25 ambapo baada ya kuona hawasikilizwi waliamua kuanzisha mgomo February 6, mwaka huu na kusababisha masomo kusimama kwa siku tatu.

Profesa Kasimoto alisema kuwa wanachuo hao wakionesha kuwa walikuwa na ajenda ya siri waligoma kumsikiliza na kukubali kuwasikiliza vinara wa mgomo huo waliokuwa wanaongozwa na mmoja wa mwanachuo ambaye alikuwa akionesha wazi kuwa ni mwanasiasa.

Alisema kuwa baada ya kuona kuwa jitihada zao za kutumia njia ya mazungumzo ya viongozi wa Serikali ya Wanachuo (TEKUSO)  kushindikana uongozi ulitoa taarifa kwa Jeshi la Polisi na ndipo vurugu kubwa zilipoibuka kuanzia katika chuo hicho hadi barabara kuu wakati waandamanaji hao wakiongozana kutaka kwenda kwa mkuu
wa mkoa.

Makamu Mkuu wa chuo alisema kuwa tabia iliyooneshwa na wanchuo hao ya kutotaka kusikiliza uongozi wa chuo na kushikilia misimamo yao huku wakitamba kuwa mabadiliko lazima, uongozi ulichukua hatua na kumsimamisha mwalimu aliyekuwa analalamikiwa.

“Unajua kama walivyotwambia sisi na hata mimi nashindwa kuelewa tatizo lao kwani kama ni mwalimu uongozi ulikwishamsimamisha   mapema tangu tulipopata malalamiko yao, kwani ni hatari kumwacha mkufunzi asiyekubalika chuoni,” alisema.

Alisema kuwa walichoshangaa ni kuona pamoja na kuuambia uongozi wa serikali ya wanafunzi kuwa mwalimu anayelalamikiwa wamekwishamsimamisha, bado wanachuo hao waliendelea na msimamo na kuzuia wenzao waliokuwa wanataka kuendelea na masomo.

Alisema kuwa baada ya mazungumzo baina yao, uongozi wa wanachuo na Mkuu wa Mkoa wamekubali kuwarudisha chuoni kwa masharti ya kufuata taratibu zilizowekwa na chuo ikiwa ni pamoja na wanachuo waliosimamishwa kutakiwa kuandika barua ya kuomba radhi na kujaza fomu maalumu.

3 comments:

  1. Naunga mkono uamuzi unaochukuliwa na Mabaraza ya vyuo kwani utavuna ulichikipanda, kuna madai ya haki kabisa wanastahili kuyadai na ndio maana wanavyuo wakaunda mabaraza yao yakiwa na Raisi,makamu nk, ili kuweza kuwasiliana na uongozi wa vyuo kutatua matatizo yao,sasa leo sera hii ya fujo inatoka wapi? Na pia mfano huyo mwanafunzi kaingia na majibu ktk mtihani ambalo ni kosa na uchunguzi kweli ukabaini katenda hilo kosa ukaamua kumsimamisha, leo eti waandamane kuulazimisha uongozi umrudishe ni kukosa maadili na pia hawana nidhamu wanastahili. Lakini wanawaadhibu baadhi ya wanafunzi wasiowafiki vitendo hivyo tatizo samaki mmoja akioza wanasababisha na wengine waoze.Naomba uongozi wa chuo ufanye uchunguzi haraka ili wabainike wale tu walioshabikia fujo wafukuzwe na waliokuwa hawakushiriki warudishwe masomini

    ReplyDelete
  2. Jamani hivi hawa vijana wa siku hizi wakoje? Yaani hawapendi amani kabisa, mawazo yao ni kufanya fujo tu, kwa nini? hivi kama wazee wao hapo zamani wangefanya vitendo kama wanavyofanya hawa vijana wa siku hizi hivi kweli Tanzania ingekuwa wapi? si ingekuwa kitu cha ajabu!! NYIE VIJANA EBU TULIENI JAMANI. MUWE WATU WA UVUMILIVU JAMANI NYIE MBONA MNATUCHOSHA. Hivi nyie wenyewe mnawaza nini hasa?

    ReplyDelete
  3. tatizo kubwa siwanafunzi tatizo ni wanasiasa kuingia mashuleni kwa nn serikali isilikemee hilo?sikuzote mwanafunzi ni mtu wa kutaka haki minimesoma ulaya shada zangu zote ukweli na ajabu ndani ya miaka karibu kumi na moja sijawahi kuona wala kusikia mwenyekiti wa chama fulani kaja au kaenda kufanya mikutano na wanafunzi serikali yetu inaliangaliaje hilo swala?ndio kiini kikubwa cha matatizo vyuoni inasikitisha sana kwa kweli naimba serikali wawe wakali na wasiliachie hilo liendelee viongozi wa siasa tunawaomba sana pamoja ya kuwa wanafunzi ni sehemu moja ya jamii wasiwatumie kihivyo bado hawana muelekeo wa maisha wenyewe wanamaisha yao na watoto wao wawaachie wasome

    ReplyDelete