23 December 2010

Pinda aenda mapumziko ya krismasi

Na Mwandishi Maalumu

WAZIRI Mkuu, Bw. Mizengo Pinda amesema Tanzania haina budi kubadili mwelekeo na kuwasaidia kwa nguvu zote wakulima wadogo ikiwa ndiyo njia ya uhakika na ya haraka ya kuondoa umasikini nchini.Bw. Pinda alikuwa akizungumza katika kijijiji cha
Inyonga, wilayani Mpanda katika siku yake ya kwanza ya ziara ya karibu wiki mbili ya Mkoa wa Rukwa jana, yakiwamo mapumziko ya krismasi.

Alisema ndiyo maana mkazo sasa unawekwa katika kuwapa wakulima wadogo, wafugaji na wavuvi, ruzuku; mbolea; pembejeo; mbegu bora na zana za kisasa.Tumebaini kuwa njia ya uhakika na ya haraka ya kuondoa umaskini wa Watanzania ni kuwasaidia wakulima wadogo, wafugaji na wavuvi. alisema.

Aliongeza: “Mkoani Rukwa tumeona mfano kwani tulipoanza kuwasaidia wakulima wadogo tumepata mazao mengi. Mwaka wa jana tulipata ziada ya tani laki saba za mazao ya chakula, mwaka huu tunaweza kupata ziada ya hata tani milioni moja.Bw. Pinda aliwasili kwa ndege Tabora jana na akasafiri kwa gari hadi Inyonga na baadaye kijijini kwake Kibaoni, katika ziara itakayojumuisha pia mapumziko ya Krismas na Mwaka Mpya.

Alilakiwa kwa shangwe Inyonga na kupongezwa kwa kuteuliwa tena, na bunge kumthibitisha kwa kura nyingi, kuwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano, baada ya uchaguzi wa Oktoba 31, mwaka huu.

Waziri Mkuu pia alisema kwamba ili kupata maendeleo ya haraka, Watanzania wote wafute ugomvi na makovu yaliyotokana na Uchaguzi Mkuu na wafanye kazi kwa pamoja bila ya kujali tofauti za vyama vya siasa, dini, rangi na ukabila.

No comments:

Post a Comment