16 December 2010

Mashoga waiwakia FIFA kuhusu ngono Uarabuni

LONDON, Uingereza
WANAHARAKATI wa haki za mashoga wamemjia juu Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu la Kimataifa (FIFA), Sepp Blatter, baada ya kusema kuwa, mashoga wanatakiwa kuacha kufanya mapenzi watakapokwenda katika fainali za Kombe la Dunia 2022
nchini Qatar, ambapo mapenzi kwa watu wa jinsia moja hayaruhusiwi kisheria.

Blatter alisema hayo baada ya kuulizwa swali na waandishi wa habari kuhusu watakavyochukuliwa mashoga wakati wa mashindano, alijibu:" Ningesema kwamba,  wanatakiwa kuacha kujishughulisha na mambo yoyote ya mapenzi."

Maoni hayo aliyatoa wakati akiwa Afrika Kusini pamoja na Rais wa nchi hiyo, Jacob Zuma, na kusababisha wanaharakati kuanza kulaumu.
Nyota wa zamani wa mpira wa kikapu katika Ligi Kuu ya Marekani (NBA), John Amaech, ambaye aliweka wazi mwaka 2007 kwamba ni shoga,  ameongoza mashambuliuzi kwa Rais wa FIFA akieleza kuwa, utamaduni huyo ni wa kizamani na ujinga.

Katika tovuti yake, alimlaumu rais huyo kwa kutoa kauli ambayo inawabana mashoga, wasagaji na waliobadilisha jinsi zao, kitu ambacho hakikubaliki.
Mtandao wa mashabiki mashoga, nao umeonesha chuki kutokana na mashindano hayo kuamriwa kufanyika Qatar ambayo ni nchi iliyo mashariki ya kati, na kumtaka Blatter kujiuzulu.

"Watu wengi (mashoga. wasagaji, waliobadili jinsi), wanaishi katika nchi ambayo wanaweza kunyongwa au kufungwa kama watabainika, watu hawa wanahitaji kusaidiwa, heshima yetu na kuungwa mkono," amesema Mwenyekiti wa kundi, Chris Basiurski katika taarifa.Aliongeza kuwa, Blatter anatakiwa kuomba radhi kwa kauli aliyotoa,  vinginevyo anatakiwa kujiuzulu kwa kauli aliyotoa.

Blatter alipotoa maoni yake katika mkutano Afrika Kusini, ilisababisha waandishi wa habari kucheka na aliongeza kuwa,  katika soka hakuna mipaka wala ubaguzi kwa binadamu.

FIFA imesema haiwezi kutoa tena maoni mengine, kwa kuwa tayari Blatter ametoa ufafanuzi katika mkutano, limesema Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC).

Blatter (74) amekuwa akitoa kauli ambazo zimekuwa zikileta tafsiri tofauti kwa watu. Aliwahi kusema mwaka 2004 kuwa, wanasoka wa kike wanatakiwa kuufanya mchezo wao kuwa maarufu kwa kuvaa 'jezi za kubana'.Mwaka huu, baada ya kutokea kashfa ya John Terry ya kufanya mapenzi na mke wa rafiki yake, aliyekuwa mchezaji mwanzake wa Chelsea, kabla ya kuhamia Manchester City, Wayne Bridge na kusababisha kuvuliwa unahodha wa England.

Alisema mchezaji huyo angekuwa katika nchi za Marekani ya Kusini,  angepongezwa (kwa kufanya mapenzi nje ya ndoa).

No comments:

Post a Comment