21 November 2010

Watatu wauawa kwa ujambazi.

Na Veronica Modest, Musoma 

WATU  watatu wanaosadikiwa kuwa ni majambazi wameuawa  na watu wenye hasira katika Kisiwa cha Nyasaungu Wilaya  ya Musoma Vijijini, mkoani Mara wakidaiwa kujiandaa kwenda
kufanya uhalifu kisiwani hapo na  mmoja anashikiliwa na jeshi la polisi.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake jana, Kamanda wa Polisi mkoa wa  Mara Robert Boaz alisema kuwa watu  hao walikuwa  wametokea Mkoani Mwanza na
kwenda kisiwani humo.

“Marehemu hao walikuwa wametokea Mwanza na walifikia kisiwani hapo Novemba 16  mwaka huu na kufikia katika nyumba ya wageni iitwayo Ikonjo  ambayo mwenyeji wao
 anaitwa Magesa Amosi,”alisema Kamanda Boaz.

Kamanda Boaz aliwataja marehemu hao kuwa ni Arute Charles (20), Mkazi wa Igoma,  Amos Alphonce (35) mkazi wa Nyakato na Abdul Seleman (37)  mkazi wa Buswelu na  anayeshikiliwa na jeshi la polisi ni Magesa Amosi Mkazi wa  kisiwa hicho.

Alisema kuwa wananchi wa eneo  hilo walianza kuwatilia mashaka marehemu hao  kuanzia siku walifika kisiwani hapo na siku ya tukio hilo  walimkuta Amos akiweka mafuta katika boti tayari kwenda kufanya  uhalifu.

“Kwa kuwa wananchi wengi wanamfahamu Amosi aliwahi kuwekwa mahabusu kuanzia  mwaka 2005 hadi mwaka 2008 kwa kosa la kunyang’anya kwa  kutumia nguvu walianza kumtilia mashaka,” alisema.

Alisema kuwa baada ya kumuona Amos akiweka mafuta katika boti ndipo wananchi  walifika na kumtaka awaoneshe wageni wake na kwenda  kuwaamusha wenzake hao na  yeye alitoroka ndipo wananchi waliwahoji watuhumiwa hao na  baada ya kuona majibu  yao hayawaridhishi waliwapiga na kuwaua.

Kamanda Boaz ametoa wito kwa wananchi wa mkoa huo kutojichukulia sheria mkononi  kwa kuwa wanaweza kuua watu ambao sio wahalifu kwa kuwa  Jeshi la Polisi lipo
katika kumaliza mtandao wa uhalifu mkoani hapo.

“Natoa wito kwa wananchi wasichukue sheria mkononi waashike wahalifu ili jeshi  letu tufanye mahojiano nao na kuwakamata wengine ambapo  itatusaidia kuharibu  mitandao yao na kuziba njia zote za uhalifu na tutaweza kupata suluhisho la muda  mrefu,” alisema.

Jeshi la Polisi lilienda kufanya upekuzi nyumbani kwa mtuhumiwa aliyesalimika na  kukuta injini mbili za boti, uchunguzi wa kina unaendelea kujua  uhalali wa
umiliki wa injini hiyo pia uchunguzi wa tukio hilo unaendelea na miili ya  marehemu imehifadhiwa katika chumba cha kuhifadhia maiti  katika hospitali ya  Mkoa wa Mara.

No comments:

Post a Comment