16 November 2010

CCM yakanusha mbunge kukimbia jimbo

Na Suleiman Abeid, Shinyanga
 
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) wilaya ya Shinyanga mjini kimekanusha uvumi kuwa mbunge aliyechaguliwa hivi karibuni katika Jimbo la Shinyanga
mjini kwa tiketi ya CCM, Bw. Steven Masele amelikimbia jimbo lake.
 
Hatua hiyo inatokana na uvumi unaonezwa na baadhi ya wakazi wa mji wa Shinyanga na vitongoji vyake kuwa Bw. Steven Masele ameamua kulikimbia jimbo hilo muda mfupi mara baada ya kutangazwa mshindi katika uchaguzi mkuu uliofanyika nchini kote Oktoba 31, mwaka
huu.
 
Matokeo hayo yalikuwa na utata na kusababisha mpinzani wa Bw. Masele aliyekuwa amegombea pia ubunge katika jimbo hilo kwa
tiketi ya CHADEMA, Bw. Philipo Shelembi kuyapinga.
 
Utata huo ulisababisha pia Msimamizi wa Uchaguzi katika jimbo hilo, Bw. Festo Kang’ombe ambaye ni Mkurugenzi wa Manispaa ya Shinyanga kutoweka kazini kwake katika mazingira ya
kutatanisha.
 
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake jana, Kaimu Katibu wa CCM wa Wilaya ya Shinyanga mjini, Bw. Saidi Bwanga alikanusha uvumi huo na kueleza kuwa wanaovumisha ni watu wasiomtakia kheri Bw. Masele pamoja na Chama chake cha
Mapinduzi.
 
“Kwa kweli mbunge wetu hajakimbia jimbo, ni uvumi tu usiokuwa na maana yoyote, wengi wanaouvumisha wanatoka katika kambi ya upinzani, ni moja ya kujaribu kuzima aibu ya kushindwa kwao, wanadai mgombea wetu hakushinda, lakini sisi tunaamini alishinda,”
alieleza Bw. Bwanga na kuongeza:
 
“Sasa wanataka kuipotosha jamii kwa kudai kuwa mbunge amekimbia jimbo, wapo wanaodai akitoka Dodoma anapitiliza Dar es Salaam, na wengine wanadai amehamishia familia yake mkoani Morogoro, madai haya si kweli, huyu bwana akitoka Dodoma atarejea Shinyanga, na pia atapita kila kata kuwashukuru wananchi,” alieleza.
 
Aidha Bw. Bwanga ambaye pia ni Katibu Mwenezi wa CCM Wilaya ya Shinyanga Mjini, amewaomba wanachama wa CCM na wapenzi wa chama hicho kupuuza uvumi huo na kwamba wajiandae kumpokea mbunge wao pale atakapokuwa akirejea kutoka Dodoma.
 
Kwa zaidi ya wiki moja sasa mji wa Shinyanga na vitongoji vyake kumezagaa uvumi kuwa Bw. Masele amehamisha familia yake kwa lengo la kulikimbia jimbo, na kwamba baada ya kuapishwa kuwa mbunge rasmi hivi sasa makazi yake yatakuwa jijini Dar es Salaam na kwamba hatua hiyo inatokana na ushindi usiokuwa wa uhakika.
 
Katika uchaguzi uliomalizika hivi karibuni Bw. Masele
alitangazwa kuwa mbunge katika Jimbo la Shinyanga mjini baada ya kupata kura 18,570 ambapo mpinzani wake Bw. Shelembi wa CHADEMA alipata kura 18,569 ikiwa ni tofauti ya kura moja.
 
Hata hivyo matokeo hayo bado yana utata kutokana na kuwepo matokeo mengine yakidai Bw. Masele alishinda baada ya kupata kura 18,750 na Bw. Shelembi alipata kura 18,507 ambayo yalipingwa vikali na mgombea wa CHADEMA akidai mshindi katika uchaguzi huo alikuwa ni yeye.
 
Kwa upande wake Bw. Shelembi alidai yeye ndiye aliyepaswa
kutangazwa mshindi baada ya kupata kura 19,231 ambapo Bw. Masele wa CCM alipata kura 19,010 matokeo ambayo yanadaiwa kupatikana kutoka katika vituo vya kupigia kura.
 
Wakazi wa jimbo hilo la Shinyanga mpaka hivi sasa wameshindwa kupata uhakika wa matokeo ya uchaguzi wa mbunge katika jimbo lao kutokana na msimamizi msaidizi katika jimbo hilo kushindwa kubandika matokeo rasmi katika mbao za matangazo kama sheria za
uchaguzi zinavyoelekeza.

3 comments:

  1. Matokeo ya kura za mbunge wa shy hayako wazi hii ni kuonyesha chama tawala wamechakachua matokeo halisi na kuwanyima wananchi wa shinyanga haki ya msingi ya kumpa ubunge mbunge waliyemtaka Bwana Phillipo Shelembi kwa mashinikizo ya watawala kwa maneno mengine masele ni mwakilishi wa viongozi wa ccm na siyo mwakilishi wa wapiga kura wa manispaa ya shinyanga.
    Rejea matokeo kutoka vituo vya uchaguzi Chama Tawala wakubali matokeo kuwa Shelembi ni mbunge halali wa Shy na siyo masele

    ReplyDelete
  2. kuna haja kutunga sheria kuhusu wasimamizi wa uchaguzi kama wakivurunda basi wafugwe hata zaidi miaa 15 na bakola mbili.

    ReplyDelete
  3. SIWEZI KUSHANGAA KAMA MGOMBEA WA CCM VUNJO NDG.MEELA ALIONGEZEWA KURA 6000 NA MSIMAMIZI WA UCHAGUZI AMEKIRI KUFANYA HIVYO KWA HIVYO SIWEZI KUSHANGAA KWA HILI LILOTOKEA NA HILI LINATHIBITISHA WAZI MADAI YA SLAA WA CHADEMA.

    ReplyDelete