07 October 2013

KASHFA GARI LA WAGONJWA GEITA NA MAPYA YALIYOFICHIKA




Ukistaajabu ya Musa utayaona na Firauni” ni maneno ambayo yamekuwa yakitumiwa na watu mbalimbali hapa nchini, yenye lengo la kuikumbusha jamii fulani juu ya yale yanayotokea kwa wakati huo.

Maneno haya, nimelazimika kuyakumbuka katika makala haya kutokana na tukio lililotokea wilayani Geita wiki iliyopita, ambapo gari la kubeba wagonjwa lilikamatwa likiwa linatumika kubeba mafuta ya wizi katika mgodi wa dhahabu wa Geita (GGM).
Kamanda wa Polisi Mkoani Geita, Leonard Paulo, anazungumzia tukio hilo kuwa lilitokea Septemba 5, mwaka huu saa saba usiku likiwa na lita 630 za mafuta zenye thamani ya sh.mil 1.3.
Analitaja kuwa ni lenye namba za usajili T.671 AKW aina ya Land Cruiser ambalo ni la kituo cha afya cha Nzera katika Halmashauri ya Wilaya ya Geita.
Anasema lilikuwa likiendeshwa na Bw.Amud Bihemo (28) ambapo lilikuwa limefunikwa maandishi yanayotoa utambulisho wake kuwa ni gari la wagonjwa kituo cha afya Nzera na mengineyo kama vile alama ya msalaba mwekundu ili lisitambulike kwa urahisi.
“Limekamatwa na polisi kwa kushirikiana na walinzi wa mgodi huo, likiwa mgodini katika eneo la kufua umeme wa mgodi lijulikanalo kama Geita power, huku maandishi yanayolitambulisha kama gari la wagonjwa Nzera yakiwa yamefunikwa kwa karatasi za mng’ao na ile sehemu ya kubebea mizigo nayo ikiwa imeng’olewa pamoja na kimulimuli chake ambapo pia waliweka kitambaa cha kuakisi mwanga ili lifanane na yale ya mgodi huo,” anasema Kamanda Paulo.
Anawataja watuhumiwa wengine ambao walikamatwa eneo la tukio kuwa ni Bw.Malemo Paul (38), Bw.Seleman Magoso (31), Bw.Julias Boas (28), Bw.Rashid Hussein (27) na Ismail Zuberi(26) wote walinzi wa kampuni ya ulinzi ya G4S.
Wengine ni Bw.Christopher Kombo(26), mfanyakazi wa mgodi huo na Joseph Christopher na kwamba watuhumiwa wengine walifanikiwa kutoroka.
Kwa hakika tukio hili, linawagusa watu wengi si wilayani humo pekee bali hata katika mikoa mingine hasa kwa wananchi waishio maeneo ya vijijini, ambao wamekuwa wakitaabika kutokana na huduma duni za usafiri pindi wanapokabiliwa na matatizo ya kiafya.
Gari hili la kubeba wagonjwa ni msaada uliotolewa na mgodi wa dhahabu wa Geita (GGM) mwezi Desemba mwaka jana, likiwa na thamani ya sh.mil. 40 ili kusaidia kuondoa kero ya wananchi wanaopata huduma ya matibabu katika kituo cha afya cha Nzera.
Kituo hiki cha afya ambacho kiko umbali wa zaidi ya kilomita 40 kufika ulipo mgodi huu, kinategemewa na idadi kubwa ya wananchi wanaoishi katika tarafa ya Bugando yenye kata sita ambazo ni Nzera, Senga, Nkome, Muharamba, Fulwe pamoja na Ruenzela.
Kwa mjibu wa sera ya afya, kituo hiki kimelenga kutoa huduma kwa wananchi wapatao 34,812 ambao ni kutoka kata ya Nzera pekee na ndio walistahili kuhudumiwa na gari hili lakini kutokana na upungufu wa magari ya wagonjwa limekuwa likitoa huduma na maeneo mengine ndani ya tarafa hii.
Baadhi ya familia zinazoishi katika maisha duni, zimekuwa zikilazimika kutumia usafiri wa baiskeli na nyingine kutumia mikokoteni inayokokotwa kwa punda ili kuwawezesha wagonjwa wao kuzifikia huduma za afya kama vile zahanati, vituo vya afya ama hospitali za wilaya na zile za rufaa.
  Usafiri wa aina hii mara nyingi umekuwa ukisababisha vifo vya mara kwa mara hasa kwa akina mama wajawazito wanapopatwa matatizo wakati wa kujifungua pamoja na watoto ambao wamekuwa wakisumbuliwa na tatizo kubwa la ugonjwa wa malaria.
   Tukio hili la gari la wagonjwa kutumika katika shughuli za wizi kinyume na matarajio ya serikali na wananchi kwa ujumla, maoni tofauti yametolewa huku mambo mapya yakijitokeza.
  Wananchi wa Nzera ndio hasa walioguswa na tukio hili kwa kile wanachokiona kuwa hali ya afya zao iko shakani kutokana na hujuma kama hizi za matumizi yasiyo sahihi ya magari ya kubeba wagonjwa.
“Taarifa hizi binafsi zilinihuzunisha mno, tumekuwa katika mateso makubwa kabla ya kuletwa katika kituo hiki, lilikuwa msaada kwetu kwani kuna familia nyingine hazina fedha kwa ajili ya kukodi gari kutoka hapa Nzera hadi hospitali ya wilaya ya Geita, hivyo lilikuwa linatusaidia kwa kweli hasa sisi kina mama,” anaeleza kwa masikitiko Bi. Verediana Nestory mkazi wa Nzera katika mazungumzo na mwandishi wa makala haya aliyetembelea kijijini hapo.
  “Tunapata shida lisipokuwepo hili gari la wagonjwa, watu wengi watapoteza maisha kwa sababu tu ya kushindwa kupata huduma mapema kutokana na kutokuwa na fedha, mfano huko nyuma kabla halijaletwa hapa kuna jirani yangu niliwahi kumshuhudia akiweka dhamana ya mbuzi ili apate gari ya kukodi toka kwa mtu binafsi ili mgonjwa wake apelekwe hospitali ya Wilaya ya Geita,” anaongeza.
  Anasema, jirani yake huyo aliyeweka dhamana ya mbuzi hakuwa na fedha kwa ajili ya kulipa usafiri wa gari ili kumuokoa binti yake aliyekuwa na tatizo la kujifungua, ambapo mumewe alimtelekeza na kukimbilia kusikojulikana.
  Mwanamke mwingine ambaye hakutaka kutaja jina lake gazetini, mfanyabiashara ya duka jirani na ulipo mgahawa aliokuwa akipendelea dereva wa gari hilo la wagonjwa kijijini hapo, anasema wao wanachotaka gari hilo lirejeshwe katika kituo hicho cha afya.
 “Kama ni wizi amefanya dereva kwa tamaa zake sawa lakini tunachotaka sisi wananchi wa Nzera, gari letu la wagonjwa waturudishie tu, kwani lilikuwa likisaidia watu wengi katika maeneo haya ya tarafa nzima ya Bugando, haiwezekani kosa afanye dereva halafu wananchi tuadhibiwe kwa kukosa huduma,” anasema.
  Baadhi ya wananchi walisema kuwa licha ya kuwa gari hilo lilitakiwa kutoa huduma hiyo bure, lakini baadhi yao walikuwa wakitozwa fedha kati ya sh.10,000 hadi 30,000 kama gharama ya kuchangia mafuta, fedha ambazo zinasadikika zilikuwa zikichukuliwa na dereva wa gari hilo.
  Kwa mujibu wa Mganga Mfawidhi wa kituo hicho cha afya Nzera, Dkt. Bahati Nyamachaguri ni kuwa kabla ya tukio hilo la kukamatwa kwa gari hilo la wagonjwa, kuna mgonjwa aliyemtaja kwa jina la Domicia Kabale (56) alikuwa amelazwa kituoni hapo na alipatwa na tatizo la kupooza mdomo ambapo alilazimika kupelekwa hospitali ya wilaya ya Geita kwa matibabu na uchunguzi zaidi.
  “Tulilazimika kulitumia gari hili la wagonjwa mimi ndiye niliongoza msafara na ndani ya gari tulikuwemo watu wanne akiwemo mgonjwa na ndugu yake, kwa kuwa kesho yake nilitakiwa kuchukua dawa za kupunguza ugonjwa wa virusi vya Ukimwi(VVU).”
  “Tulifika salama saa 11 hivi jioni ya siku hiyo, mgonjwa akapokelewa na wenzetu wa hospitali ya wilaya na kwa mujibu wa sheria niliamini gari hilo litabaki hapo hospitali hadi kesho yake,” anaongeza.
  Anasema, kesho yake asubuhi wakati anafika hospitalini hapo akijiandaa kwenda kuchukua dawa hizo lili arudi kituoni kwake kwa kulitumia gari hilo, alishangaa baadhi ya madereva waliokuwa wamekusanyika wote wakiwa wameelekeza macho yao kwake na baadaye aliambiwa kuwa gari la kituo chake cha Nzera liko kituo cha polisi baada ya kukamatwa likifanya uhalifu mgodini.
  “Nilienda kituoni pamoja na mkurugenzi, tulikuta kweli gari liko hapo polisi, likiwa limezibwa maandishi kwa stika, sehemu ya juu ya kubebea mizigo imeng’olewa na imewekwa kitambaa cha mng’ao kama yale ya mgodini, nilibaki kushangaa.” anasema.
  Mganga huyo Mfawidhi, anasema gari hilo huwa linawekewa mafuta kila siku ya Jumatatu kutoka ofisi ya Halmashauri ya wilaya na kuwa tukio hilo alilosema kuwa siyo zuri limemuumiza yeye binafsi.
 “Kwa kweli limenipatia fundisho kubwa wananchi walikuwa wamelizoea kutokana na kuwa msaada wao mkubwa ingawa wapo baadhi ya viongozi wa kisiasa walikuwa wakitoa vitisho kwa dereva pindi anapogoma kufanya yale wanayotaka ikiwemo kubeba wagonjwa wao pasipo kupitia ngazi zinazohusika za uongozi. Hii inatokana na baadhi ya watu kutojua utaratibu.
  Mwandishi wa makala haya akiwa kituoni hapo, alishuhudia mume na mke waliokuwa na mtoto wao aliyekuwa na tatizo la kuishiwa damu kwa mjibu wa daktari, wakibaki kuangua kilio kutokana na kushindwa gharama ya nauli ya sh.4,000 ili kumfikisha mtoto huyo hospitali ya wilaya ya Geita kwa matibabu.
  Majira iliweza kubaini kuwa katika kituo hicho, hapakuwepo na kitabu cha makabidhiano kwa ajili ya kusaini pindi gari hilo linapoingia ama kutoka ambapo dereva wake pia hakuwa mtumishi wa kudumu wa Halmashauri hiyo bali alikuwa akifanya kazi kama kibarua (cassual) aliyekuwa akisaini mkataba kila baada ya miezi mitatu.
  Mmoja wa dereva basi dogo la abiria maarufu kama Hiace linalofanya safari zake kutoka mjini Geita kwenda Nkome kupitia kijijini hapo, ambaye hakutaka kutaja jina lake kwa usalama wake, anasema mara nyingi gari hilo la wagonjwa amekuwa akilikuta limeegeshwa porini jirani na eneo la mgodi wakati wa usiku.
  “Hawa bwana watakuwa wamedhulumiana wao kwa wao tu ni mara nyingi pengine limekuwa likitumika kwa shughuli kama hizi hasa usiku, nimekuwa nikikutana nalo limeegeshwa hapa porini usiku, siku zimefika mwisho, dogo amechezea kazi ningelikuwa na ndugu yangu huko wizarani ningelimpigia nipate hiyo nafasi,” anasema.
  Naye mlinzi mmoja wa kampuni ya Intensive Security inayotoa huduma ya ulinzi katika hospitali ya wilaya ya Geita(jina limehifadhiwa), anasema siku ya tukio dereva huyo aliwaeleza kuwa yuko zamu ya usiku, hivyo gari lake litakuwa na mizunguko ya mara kwa mara kutoka nje na kuingia lango kuu la hospitali hiyo ya wilaya.
  “Unajua bwana yaani unaweza kudanganya sana lakini kama siku imefika imefika tu, siku hiyo alikuja hapa getini na kutueleza yuko zamu na kama kawaida tuna vitabu huwa tunaweka kumbukumbu yaani siku hiyo alianza kutoka saa 2 usiku na kuingia mara nyingi kweli hadi tukachoka kufungua geti tukalazimika kuliacha wazi na mara ya mwisho alitoka saa 7 usiku,”anasema mlinzi huyo wa Kampuni ya Intensive Security na kuwa kuruhusiwa kwa gari hilo kunatokana na magari ya wagonjwa wakati mwingine kutumika kuwapeleka madaktari nyumbani kwao pindi wanapomaliza kazi za kuhudumia wagonjwa.
Mkuu wa Mkoa na wilaya nao wanena
    Mkuu wa Mkoa wa Geita, Bw. Magalula Said Magalula, katika mazungumzo na waandishi habari ofisini kwake, amewataka madereva na viongozi wa serikali kuacha kutumia vibaya mali ya umma kwa kuwa ni aibu.
   Mkuu wa Wilaya ya Geita, Bw. Manzie Omary Mangochie, anasema tukio hilo limemshtua mno na kwamba hakuwa na mawazo kuwa kuna siku ataliona gari la wagonjwa likiwa linatumiwa katika vitendo vya wizi badala ya kufanya kazi yake ya kubeba wagonjwa.
  “Nimesikitika sana, binafsi nimelazimika kufika kituoni mwenyewe kuona kitendo hiki cha fedheha! Lazima hatua zichukuliwe kamwe hatutokubali vitendo vya namna hii viendelee katika wilaya yetu, nimeagiza hatua kali zichukuliwe mara moja,”anasema mkuu huyo wa wilaya kwa masikitiko makubwa.
Kauli ya uongozi wa Halmashauri
  Kwa upande wake Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Geita, Bw. Ali Kidwaka, anakiri kuwa ni kweli dereva huyo alikuwa kibarua kwa muda wa mwaka mmoja sasa.
“Niliunda timu maalumu kufuatilia mara baada ya tukio hili na ilifahamika dereva hakuwa mwajiriwa wa kudumu wa Halmashauri, lakini pia limetupatia fundisho na angalizo kubwa,” anasema.
 “Gari la wagonjwa kutumika katika wizi kama huu bila shaka hata wewe mwandishi hili wazo sidhani kama ulikuwa nalo kuwa inaweza kuwa, ndivyo hivyo hata mimi lakini kuanzia sasa tunaanza kufanya ufuatiliaji magari yote ya serikali katika Halmashauri, tutatoa waraka kama njia ya kudhibiti na kweli tutafanya hata ziara za kushtukiza,” anaongeza.
  Anasema, kwa sasa Halmashauri hiyo yenye vituo vya afya vitano ambavyo ni Katoro, Chikobe, Kashishi, Bukoli na Nzera inakabiliwa na upungufu mkubwa wa magari ya kubeba wagonjwa ambayo yaliyopo sasa ni mawili pekee.
  Kwa mjibu wa taarifa ya maombi maalumu yaliyopelekwa Wizara ya Fedha kwa Halmashauri hiyo mwaka 2011, jumla ya sh.mil. 420 zilikuwa zimeombwa kwa lengo la kununua magari matatu ya kubeba wagonjwa, maombi ambayo hayakukubaliwa.
  Maombi hayo yalikuwa yamelenga kurahisisha utoaji wa huduma kwa haraka ikiwa ni pamoja na kuokoa maisha ya wananchi wilayani humo.
Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo, Bw.Elisha Lupuga anasema “dereva huyu lazima afukuzwe kazi mara moja na kutokana na tukio hili jana tumefanya kikao na madereva wote wa Halmashauri, tumeonya kuwa endapo litajirudia hatutawafumbia macho wale wote watakaopatikana wakijihusisha na vitendo hivi,” anasema.
  “Suala la kwamba dereva alikuwa mwajiriwa wa muda si hoja bali hata kama angelikuwa ameajiriwa angefanya hivyo kama ni tabia yake, hivyo lazima hatua zichukuliwe kwa mujibu wa sheria,” anaongeza mwenyekiti huyo.
Viongozi wa vyama vya siasa wanazungumziaje tukio hili?
  Katibu wa Itikadi, Siasa na Uenezi wa Chama Cha Mapinduzi(CCM) mkoani Geita, Bw.Said Kalidushi anasema kuwa tukio hilo ni sawa na hujuma kwa wagonjwa ambao ndio wanaolitegemea zaidi.
  “Ni hujuma kwa wagonjwa, mfano endapo pangelikuwepo na mgonjwa ambaye alitakiwa kutolewa kituoni hapo kwenda hospitali ya wilaya ya Geita kwa matibabu zaidi ina maana angelipoteza maisha kutokana na hujuma kama hizi.”
  “Siamini inakuwaje gari la wagonjwa liende mgodini kuiba mafuta badala ya kuhudumia wagonjwa? CCM imekuwa ikilalamikiwa kwa matukio kama haya, hizi ni tamaa zake na gari hili lilitolewa na mgodi na hilo hilo ndilo limeenda kuiba humo ndani yaani hii ni sawa na mbwa anayemng’ata mfugaji wake...” anasema na kuongeza kitendo hicho kisiwavunje wafadhili bali waendelee kutoa misaada kwa jamii pale wanapoona inafaa kuwa hivyo.
Msemaji wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) mkoani Geita, Ignas Karashani, anasema kuwa serikali inatakiwa kufanya uchunguzi wa kina ili kubaini endapo kitendo cha gari hilo kwenda kufanya wizi mgodini kilikuwa na shinikizo toka kwa kiongozi yoyote ili hatua zichukuliwe mara moja.
  “Kazi ya gari hili ni kubeba wagonjwa kwa dharura, huko nani aliamuru liende? Pale Nzera kuna diwani ambaye ni Musukuma kama diwani naye alipaswa kufuatilia kwa karibu kwa sababu linahudumia watu wake, lazima naye ahojiwe huenda alishinikiza kwa maslahi yake,” anasema Diwani wa kata ya Nzera ambaye pia ni Mwenyekiti wa CCM mkoani humo, Bw.Joseph Musukuma yeye alitupia lawama Mganga Mfawidhi wa kituo hicho pamoja na dereva kuwa wanastahili kuwajibika.
  “Mganga Mkuu na dereva wote wanatakiwa kwenda jela tu hao,” alimaliza kisha kukata siku kwa kile alichoeleza alikuwa akiendelea na mkutano.
Uongozi wa mgodi
  Kaimu Mkurugenzi Mgodi wa Dhahabu wa Geita (GGM), Bw. Jasper Musadaidzwa, katika taarifa yake kwa vyombo vya habari anasema kuwa mgodi huo umeshtushwa na tukio hilo la wizi uliofanywa kwa kutumia gari la kubeba wagonjwa.
  Anasema, mgodi huo ulitoa msaada wa gari hilo, kwa lengo la kusaidia kusafirisha wagonjwa, watoto na akina mama wajawazito kwa kuzingatia moja ya sera ya afya ya mgodi huo isemayo wananchi lazima wanufaike na uwepo wao.
  “Tumeshtushwa na wizi huu ambao umefanywa na watu wachache ambao wanatumia rasilimali za umma kwa matumizi yao binafsi badala ya kuokoa maisha ya watu,” anasema mkurugenzi huyo wa GGM.
  Kukamatwa kwa gari hilo la wagonjwa likiiba mafuta mgodini humo, kumeleta hofu kubwa kuwa huenda pengine yapo baadhi yanatumika katika usafirishaji dawa za kulevya kwa kuwa si rahisi kukaguliwa na polisi kwa kudhaniwa yamebeba wagonjwa.
  Takwimu zinaonesha kuwa Tanzania inakabiliwa na uhaba mkubwa wa magari ya kubeba wagonjwa katika vituo na hospitali mbalimbali, hali ambayo ilisababisha Rais Jakaya Kikwete wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu 2010, kuahidi kusambaza pikipiki za matairi matatu (bajaji) zipatazo 400,000 nchini.
  Katika ahadi hiyo, Rais Kikwete alisema lengo ni kusaidia wagonjwa hususani wanawake wajawazito kuwahishwa hospitali wakati wa kujifungua.
  Kwa mujibu wa sera ya afya ya mwaka 2007, Serikali kwa kushirikiana na wadau mbalimbali itahakikisha utoaji wa huduma bora za uzazi katika vituo vya kutolea huduma za afya zinazowavutia wanawake, wanaume na vijana hapa nchini.
.

No comments:

Post a Comment