03 September 2013

WATUHUMIWA DAWA ZA KULEVYA WAKIMBIA




 Na Rehema Mohamed
MAHAKAMA Kuu Kanda ya Dar es Salaam, imetoa amri ya kukamatwa wadhamini wawili waliowadhamini raia wawili wa Pakistan waliokuwa wakikabiliwa na kesi ya kukutwa na dawa za kelevya kinyume cha sheria ili waitwe mahakamani na wajieleze baada ya washtakiwa waliomdhamini kukimbia.
Wadhamini hao ni Amiral Sharif, mkazi wa Kisutu na Elias Kumrudin, mjumbe wa nyumba 10 Mtaa wa Libya
.Wengine ni Mohamed Bahishi, mkazi wa Chang'ombe, Dar es Salaam na Nazar Mohamed Nuru, mkazi wa Mtaa wa Libya, Kisutu, Dar es Salaam, ambao ni waajiriwa wa kampuni ya Songea Mining & Construction Ltd Holdings.
Amri hiyo ilitolewa jana mahakamani hapo na Jaji Grace Mwakipesile, baada ya washtakiwa hao na wadhamini wao, kutokutokea mahakamani kwa ajili ya kusikiliza kesi yao.Mahakama hiyo pia imetoa hati ya kuwakamata washtakiwa hao, ili kufikishwa mahakamani kuendelea na kesi inayowakabili.
Washtakiwa waliokimbia ni Abdul Ghan Bux na Shahbaz Malik, pamoja na Watanzania wawili Fredy William Chande na Kambi Seif ambao wanakabiliwa na mashtaka ya kula njama na kuingiza dawa za kulevya nchini kinyume cha Sheria ya Kuzuia Usafirishaji na Biashara ya Dawa za Kulevya.
Katika kesi hiyo namba moja ya mwaka 2012, washtakiwa hao wanadaiwa kuingiza nchini dawa hizo aina ya heroin ambazo zinadaiwa kuwa na thamani ya sh. bilioni 6.Kesi hiyo ilitarajiwa kuanza kusikilizwa jana hatua ya awali ambapo washtakiwa hao wangesomewa maelezo ya awali juu ya mashtaka yanayowakabili, lakini ilikwama kusikilizwa baada ya washtakiwa wawili (Wapakstani) kutokomea kusikojulikana.
Kutokana na hali hiyo, Wakili wa Serikali Theophil Mutakyawa, alidai kesi ilipangwa kwa ajili ya usikilizwaji wa awali lakini aliiomba mahakama itoe amri ya kukamatwa washtakiwa na wadhamini wao kwa kutofika mahakamani.Alidai kumbukumbu zinaonesha Julai, 2011, washtakiwa wote walipewa dhamana na mahakama hiyo hivyo mshtakiwa wa tatu na nne, wamekiuka masharti ya dhamana kutokufika mahakamani.
"Katika mazingira haya ni rai ya Jamhuri kwamba itolewe hati ya kuwakamata washtakiwa namba tatu na nne ili waweze kufika kwa tarehe itakayopangwa, pia itolewe hati ya wito wa mahakama kwa wadhamini wao waje wajieleze," alidai Mutakyawa.
Jaji Mwakipesile, alipomuuliza Wakili wa washtakiwa hao, Yassin Membar, alijibu hana taarifa zozote za washtakiwa hao hivyo alikubaliana na maombi ya Jamhuri kuamuru washtakiwa hao wakamatwe na samansi kwa wadhamini wao kama upande wa mashtaka ulivyoomba.Kesi hiyo iliahirishwa hadi tarehe nyingine itakayopangwa na Msajili wa Wilaya wa Mahakama Kuu.
Washtakiwa hao wanadaiwa kwa nyakati tofauti kati ya Januari mosi na Februari 21, 2011 katika maeneo tofauti nchini na Pakistani, walikula njama na kutenda makosa ya kusafirisha, kuingiza nchini dawa za kulevya.Inadaiwa walikamatwa Februari 21, 2011, Mtaa wa Jongoo eneo la Mbezi Beach, Dar es Salaam, wakiwa na dawa hizo zenye uzito wa gramu 179,000 zenye thamani ya sh. bilioni 6.2.
Wakati kesi yao hiyo ikiendelea katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, katika hatua za awali, washtakiwa hao waliwasilisha Mahakama Kuu, Dar es Salaam, maombi ya dhamana.Wakati maombi hayo yakisikilizwa, upande wa utetezi ulidai hakuna uthibitisho wa thamani ya pesa za dawa hizo kwani hakuna hati inayothibitsha thamani hiyo.
Mawakili wa utetezi walidai hata hati ya mashtaka haielezi ni nani aliyetuma dawa hizo kutoka Pakistan na aliyezipokea nchini.Waliongeza kuwa, hati ya mashtaka haikueleza taarifa binafsi za washtakiwa kama umri na utaifa wao hivyo kutokana na dosari hizo washtakiwa wana haki ya kupewa dhamana.
Baada ya kusikiliza hoja za pande zote, Julai 6, 2011, Jaji Upendo Msuya aliwapa dhamana, akisema upande wa mashtaka ulishindwa kuthibitisha sababu za kuwanyima dhamana baada ya ukikiri kutowasilisha nyaraka muhimu za kutetea hoja zao.

1 comment:

  1. Hawa kwanini walipewa dhamana? Taifa linataka majibu toka mahakamani waliotoa hiyo dhamana, tukumbuke kuna wanachi hawapewi dhamana je hawa pk walipata vipi dhamana na hali ni wageni? Ina maana hapa kuna mchezo mchafu ambao mahakama inauelewa

    ReplyDelete