Livinus Feruzi na
Theonestina Juma, Kagera
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) mkoani
Kagera, kimetetea uamuzi uliofikiwa na Halmashauri Kuu ya chama hicho Mkoa wa
kuwafukuza uanachama madiwani nane na kudai kuwa, uamuzi huo utaendelea
kuheshimiwa.
Mwenyekiti wa CCM mkoani humo, Bi.
Constancia Buhiye, aliyasema hayo jana wakati akizungumza na waandishi wa
habari siku chache baada ya Katibu wa NEC, Itikadi na Uenezi wa chama hicho
Taifa, Bw. Nape Nnauye, kusema uamuzi huo hauna baraka ya vikao vya ngazi ya
juu katika chama hicho.
Bi. Buhiye alisema kwa mujibu wa katiba
na kanuni ya CCM, Halmashauri Kuu ya chama hicho ndiyo kikao cha mwisho katika
maamuzi ya kuwawajibisha wanachama wake ngazi ya Mkoa.
Alisema maamuzi yaliyofikiwa na
Halmashauri Kuu ya CCM mkoani humo ya kuwafukuza uanachama madiwani hao ni halali
na yataendelea kuheshimiwa hadi hatua nyingine zitakapofikiwa kama rufaa ya
madiwani hao au ushauri wa vikao vya juu.
"Kwa kutumia katiba hii na kanuni
hii, Halmashauri Kuu ya CCM ni chombo chenye haki ya kusimamisha uanachama
wanachama wake," alisema Bi. Buhiye.
Aliongeza kuwa, vikao vya juu katika
maamuzi yake pia vitarejea katiba na kanuni ya chama na kuwataka wana CCM Mjini
Bukoba kuwa watulivu, wavumilivu na kuheshimiana ili kuepuka suala zima la
uvunjifu wa amani.
"Mimi sipingani na Nape na sitaki
kuamini niliyoyasikia kutoka kwa watu wengine maana mimi binafsi sikusikia
lakini katika katiba yetu, hakuna kikao kinachofuta maamuzi ya kikao kingine,
kila kikao ni halali," alisisitiza Mwenyekiti huyo.
Aliongeza kuwa, "Halmashauri Kuu
ni kikao halali na maamuzi ni halali ambayo yataendelea kuheshimika."
alisema na kudai kuwa, baada ya kikao hicho maamuzi yaliachwa kwa Mtendaji Mkuu
wa chama ili kuandaa taarifa iweze kutumwa katika ngazi husika na kuwapatia
barua madiwani hao.
Alisema hadi sasa ofisi yake haina taarifa za maandishi
zilizotolewa na viongozi wa ngazi za juu kuhusu suala hilo.
No comments:
Post a Comment