15 July 2013

MAUAJI DARFUR


  • JWTZ WATHIBITISHA
 Na Rehema Mohamed
JESHI la Ulinzi la Wananchi wa Ta n z a n i a ( JWT Z ) , limethibitisha kuuawa kwa wanajeshi saba na wengine 14 kujeruhiwa vibaya akiwemo askari polisi mmoja wote kutoka Tanzania baada ya kushambuliwa na waasi.
Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Msemaji wa jeshi hilo nchini, Kanali Kapambala Mgawe, alisema wanajeshi hao ni miongoni mwa askari wanaolinda amani kwenye Kikosi cha Umoja wa Mataifa (UN), Mjini Darfur, nchini Sudan.
Alisema wanajeshi hao waliuawa katika shambulio la kushtukiza ambalo lilifanywa na waasi hao Julai 13, mwaka huu, saa 3 asubuhi, wakati wakiwasindikiza waangalizi wa amani kutoka Khor Abeche kwenda Nyara mjini humo

.
Shambulio hilo lilitokea umbali wa kilomita 20 kutoka Makao Makuu ya Kikosi hicho ambapo miongoni mwa waliojeruhiwa ni pamoja na Maofisa na askari kutoka mataifa mengine.
Aliongeza kuwa, wakati kikosi cha wanajeshi wa Tanzania kikishambuliwa, kilikuwa na askari 36 lakini hakuwa tayari kutaja majina ya wanajeshi waliouawa.
"Hatuwezi kutaja majina ya wanajeshi waliouawa kwani ni mapema mno, tusubiri taratibu nyingine za kijeshi zikamilike, kwa sasa mazingira ya ulinzi Mjini Darfur, yanafanyika kwenye daraja sita ambayo si ya kutumia silaha.
"Kutokana na shambulio hili, tunafanya mawasiliano na UN waruhusu matumizi ya daraja la saba ili kuongeza uwezo zaidi wa kujilinda na mashambulizi pale askari wanaposhambuliwa na waasi," alisema Kanali Mgawe.
Alisema vifo hivyo vimeisikitisha JWTZ kwani tukio hilo limetokea katika mazingira ya ulinzi wa amani ambao hauna matumizi ya silaha.
"Hii ni taarifa ya awali juu ya tukio hili...baada ya tukio hili kikosi chetu Mjini Darfur kilitoa taarifa Makao Makuu Dar es Salaam, miili ya marehemu na majeruhi iliondolewa eneo la tukio na kupelekwa Nyara ambako kuna Hospitali Kuu ya eneo la operesheni kwa taratibu za matibabu," alisema.
Kanali Mgawe alisema, JWTZ linawasiliana na familia za marehemu juu ya taratibu za mazishi pamoja na UN kuhusu taratibu zote muhimu zinazohusiana na matibabu ya wanajeshi waliojeruhiwa katika eneo la tukio.
Katika hatua nyingine, Kanali Mgawe alisema tayari ujumbe maalumu umeteuliwa kwenda Khartom, Darfur kuzungumza na mamlaka husika kuhusu shambulizi hilo.
Jumla ya askari 875 wa jeshi hilo waliondoka nchini Februari mwaka huu kwenda Sudan ili kulinda amani chini ya Mpango wa Kulinda Amani wa Umoja wa Mataifa.

No comments:

Post a Comment