21 January 2013

Tusikemee rushwa bila wahusika kukamatwa, kuchukuliwa hatua



TATIZO la rushwa nchini, lipo katika sekta mbalimbali lakini hali hiyo haina maana kuwa inakubalika katika jamii.

Ukweli ni kwamba, rushwa haikubaliki kutokana na madhara yake ndio maana Serikali imeweka mikakati mbalimbali ya kuhakikisha vitendo hivyo vinatokomezwa.


Rushwa inaathiri maendeleo ya mtu binafsi, familia, Taifa, kushusha hadhi ya mtoaji na mpokeaji. Rushwa inachangia kupindisha kanuni za maadili wakati wa kutekeleza majukumu kwa masilahi ya umma, mtu au kikundi fulani.

Vitendo hivyo vinajumuisha matumizi mabaya ya madaraka na kusababisha baadhi ya viongozi wa umma na sekta binafsi, kutumia dhamana walizonazo kinyume cha sheria ili kujinufaisha.

Rushwa imebatizwa majina mengi, ambapo watu wanaojihusisha na vitendo hivyo, huwanyima wananchi mategemeo ya kuwa na maisha bora, kuwakosesha elimu, huduma bora za afya, chakula, maji na mahitaji mengine ya kibinadamu.

Sisi tunasema kuwa, rushwa ni wizi dhidi ya Taifa na wananchi ambao wanategemea kupata maisha bora, inachochea makosa ya jinai yanayovuka mipaka, kuvunja amani na utulivu.

Rushwa ina madhara makubwa kiuchumi kwa lugha nyepesi ni
uovu unaowavunja moyo Watanzania na wafanyabiashara
ambao wangependa kuwekeza nchini.

Inaongeza ugumu wa maisha kwa wananchi wakati mwingine hucnagia kupunguza ubora wa bidhaa zinazozalishwa viwandani.

Imani yetu ni kwamba, rushwa husababisha mapato ya Serikali Kuu na Serikali za Mitaa kupungua hivyo kupuguza uwezo wa kutoa huduma kwa wananchi kutekeleza malengo ya kuboresha maisha yao na miundombinu ya nchi.

Uovu wa rushwa unachangia kuongeza umaskini katika jamii, kuathiri ubora wa elimu na sekta nyingine nchini.

Rushwa inaweza kusababisha mgonjwa asipone haraka au kupoteza maisha kama mgonjwa atakataa au kukosa kile alichodaiwa kukitoa.

Tukifikia kiwango cha kuibubali rushwa kama sehemu ya utamaduni wetu, waathiriwa wataamua kujilinda wenyewe kwa kuchukua sheria mkononi hivyo kuharibu sifa ya amani na utulivu tulionao.

Viongozi mbalimbali wa Serikali wamekuwa wakikemea vitendo vya rushwa bila wahusika kukamatwa na kufikishwa katika vyombo vya sheria ili iwe fundisho kwa wengine.

Hali hii inachangia jamii kubwa kypambana na rushwa kwa mazoea kutokana na mfumo unaotumika kuitokomeza.

No comments:

Post a Comment