20 December 2012

Mwongazo wa Taifa utaboresha mafunzo ya ujasiliamali-NEEC


Na Grace Ndossa

KATIBU Mkuu Mtendaji wa Baraza la Taifa la uwezeshaji wananchi kiuchumi(NEEC)Dkt.Anacleti Kashuliza amesema kuwa baada ya mwongozo wa Taifa  wa mafunzo ya ujasiriamali kupitishwa hakuna chuo kitakachoruhusiwa kutoa mafunzo ya ujasiriamali bila ya kufuata mwongo.

Dkt.Kashuliza  alitoa kauli hiyo  Dar es Salaam jana wakati wa warsha ya siku moja ya kupata maoni ya wadau kuhusu mwongozo wa taifa  wa mafunzo ya elimu ya ujasiriamali.

"Tunataka viwango vinavyofanana kutoa mhitimu  mahiri kwani wengi wanakuwa wakihitimu mafunzo ya ujasiriamali, wanakuwa hawawezi kufanya shughuli zao vizuri,"alisema Dkt.Kashuliza.

Alisema kuwa mwongozo huo ndio utawezesha nchi iweze kuzalisha  wajasiriamali  kwani watahimili soko la ushindani na wengine kuzalisha bidhaa ambazo zinaweza kupelekwa nchi nyingine.

Alisisitiza kuwa baada ya mwongozo kupitishwa wale ambao hawatakuwa na uwezo wa kufuata  watafute shughuli nyingine za kufanya.

Aliwataka wadau waanze  kujipanga kwa ajili ya kutumia mwongozo huo hatua itakayoondoa hali ya sasa ya watu kutoa mafunzo ya ujasirimali lakini  hayafanani na mengine ni duni.

Awali Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Elimu Tanzania Dkt.Paul Mushi akizindua mwongozo huo kwa niaba ya Waziri wa Elimu na mafunzo ya Ufundi Dkt. Shukuru Kawambwa alisema kuwa mwongozo huo utasaidia kuhakikisha  kuwa utekelezaji wa elimu ya ujasirimali umezingatia maeneo muhimu ya Kitaifa na watoa elimu wote ili kuwezesha watanzania kujikomboa kielimu na kiuchumi.

Alisema kuwa  mwongozo huo  umeandaliwa ili kutoa  mwelekeo katika mbinu na matokeo ya ujifunzaji mbinu za upimaji,utahini na sifa za mwezeshaji  zinazotakiwa, kwani viwango hivyo vitasaidia  kuongoza mafunzo na kupima matokeo ya ujifunzaji kwa ufanisi.

Pia alisema mwongozo huo  umebaini na kutenganisha  mfumo rasmi na usio rasmi katika kutoa mafunzo kuhusu elimu ya ujasiriamali, lengo ni kuwezesha  walengwa waweze kutumia muktadha na  kujenga maarifa  na mwelekeo kulingana na mazingira ya  kutolea elimu.

No comments:

Post a Comment