23 November 2012

Dkt. Mwakyembe 'aikoromea' Bodi Mpya TPA



Na Mashaka Mhando, Tanga

WAZIRI wa Uchukuzi, Dkt. Harrison Mwakyembe, amesema Wizara hiyo itasaini mkataba wa miezi sita na Bodi ya Mamlaka
ya Usimamizi wa Bandari nchini (TPA), aliyoichagua hivi karibuni na kama itashindwa kufikia malengo waliyopewa itaondolewa.


Dkt. Mwakyembe aliyasema hayo jijini Tanga wakati akizungumza na waandishi wa habari na kusisitiza kuwa, Wizara yake imeanzisha utaratibu mpya wa kuingia mikataba na bodi ili kuleta ufanisi.

Alisema baada ya kuivunja bodi ya awali na kuchagua mpya, tayari kamati ya uchunguzi imepeleka taarifa na mapendekezo mbalimbali ambayo ndio yalisaidia kuundwa kwa bodi hiyo yenye wajumbe wanane ikiongozwa na Bw. Raphael Mollel.

“Mapendekezo ya kamati juu ya tuhuma mbalimbali kwa waliokuwa wafanyakazi na wajumbe wa bodi, Wizara haitamuonea mtu yeyote bali tutakuwa na maamuzi yenye lengo la kuboresha Bandari ya Dar es Salaam iweze kukabiliana na changamoto mbalimbali.

“Lengo ni kuondoa vigigi vilivyopo, mapendekezo ya kamati ndio yaliyochangia kuundwa kwa bodi hii yenye vijana wenye umri kati ya miaka 45 na mmoja mwenye miaka 65,” alisema.

Aliisifu bodi mpya na kudai wajumbe wake ni vijana wazalendo wenye sifa zinazokubalika hivyo anaamini watafanyakazi zao kwa weledi ili kufikia malengo yaliyokusudiwa na Wizara katika kipindi kifupi kijacho.

“Kuna baadhi ya watendaji pale Bandari ya Dar es Salaam wanatuharibia hivyo lazima tufikie malengo yetu na kutoa
ushindani katika bandari nyingine ili tuwe kimbilio la wengi,”
alisema.

Dkt. Mwakyembe ambaye aliongozana na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Dkt. Omari Chambo na Mkurugenzi Mkuu wa Usafirishaji Bw. Peter Lupatu, alifuta utaratibu wa watendaji waliopo chini ya Wizara yake kukata tiketi za daraja la kwanza badala yake wanaposafiri nje ya nchi kwa usafiri wa ndege badala yake wakate za daraja la pili.

“Watendaji ambao watakasirika waende mahakamani, nasema hivi kama utaratibu wa kupanda daraja la kwanza upo katika mikataba yenu ya ajira naifuta rasmi kuanzia leo (jana),” alisema.

Aliongeza kuwa ni bora zinazotumika kwa ajili ya watendaji hao
kusafiia daraja la kwanza zikatumika kuboresha mazingira ya shule zilizopo nchini na kujenga matundu ya vyoo ili wanafunzi waondokane na tatizo hilo.

No comments:

Post a Comment