23 August 2012

DC Serengeti afariki, Rais Kikwete amlilia


Na Veronica Modest, Musoma.

MKUU wa Wilaya ya Serengeti, Bw.James Lyamungu, amefariki dunia katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH) jijini Dar es Salaam alipokuwa akipatiwa matibabu.

Kutokana na kifo hicho, Rais Jakaya Kikwete, amemtumia Mkuu wa Mkoa wa Mara, Bw.John Tupa, salamu za rambirambi kuomboleza kifo cha Bw.Yamungu kilichotokea alfajiri ya jana MNH.


Katika salamu hizo, Rais Kikwete amemwambia, Bw.Tupa kuwa, amepokea kwa huzuni na mshtuko taarifa za kifo chake.

"Kifo cha Kapteni Yamungu kimeinyang'anya nchi yetu na Serikali yetu mtumishi hodari na mwadilifu wa umma ambaye katika utumishi wake wote tokea alipokuwa Jeshi hadi anaingia uongozi wa siasa alithibitisha uaminifu wake kwa nchi yetu na uongozi wake," alisema Rais Kikwete na kuongeza;

"Napenda kuwajulisheni kuwa moyo wangu uko nanyi katika kipindi hiki kigumu. Nawaombea uvumilivu na subira na naungana nanyi kumwomba Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema, aiweke pema peponi roho ya Marehemu James Charles Yamungu, Amen."

Bw.Tupa alisema marehemu alikuwa mchapakazi na atakumbukwa kwa mchango wake.






No comments:

Post a Comment