11 June 2012
Kamati Miss Tz kuwafunda Kigamboni
Na Mwandishi Wetu
KAMATI ya Miss Tanzania kesho inatarajia kukutana na wanyange wanaowania taji la kitongoji cha Kigamboni 'Miss Kigamboni 2012' kwa ajili ya kuwafunda na kufahamu taratibu na malengo ya mashindano hayo.
Mashindano hayo ya Kigamboni, yanatarajia kufanyika Juni 15, mwaka huu katika Ukumbi wa Navy Beach kuanzia saa 1 usiku.
Akizungumza Dar es Salaam jana, Mratibu wa mashindano hayo, Somoe Ng'itu alisema warembo hao pia watapata nafasi ya kuuliza maswali mbalimbali kuhusiana na tasnia hiyo ambayo mshindi wake kitaifa hupata nafasi ya kuiwakilisha nchi katika mashindano ya Dunia.
Alisema maandalizi ya mashindano hayo yanaendelea vizuri na kila mshiriki amejigamba kuondoka na taji.
Somoe alisema wanawaomba wakazi wa Kigamboni na wengine kutoka sehemu mbalimbali jijini kujitokeza kushuhudia warembo wao, ambao baadaye watakwenda kukiwakilisha kitongoji hicho kwenye mashindano ya Kanda ya Temeke.
Alisema katika fainali hizo bendi muziki wa dansi ya FM Academia 'Wazee wa Ngwasuma' na msanii wa vichekesho Mpoki ambaye ni mkazi wa Kigamboni watatoa burudani ya aina yake.
Aliwataja warembo wanaojiandaa kuwania taji hilo kuwa ni Carolyne Dandu, Fatina Francis, Edda Slyvester, Aisha Mussa, Rosemary Peter, Doreen Kweka, Carolyne Peter, Agnes Goodluck, Sophia Martine, Rosemary Deogratius, Beatrice Boniface, Julieth Philip, Khadija Kombo na Winnie Karaya.
Alisema mashindano hayo yanadhaminiwa na a Kampuni ya Bia Tanzania (TBL) kupitia kinywaji chake cha Redd's, Dodoma Wine na NSSF.
Wengine ni Times FM Hope Country Motel, Norbro’s Collections na Screen Masters.
Alisema warembo watakaofanya vizuri watachuana na wenzao wa Chang'ombe na Kurasini kuwania taji la Kanda ya Temeke.
Subscribe to:
Post Comments (Atom)

No comments:
Post a Comment