25 May 2012

Kesi ya kupinga matokea zisifunguliwe kwa jazba



JANA Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam,ilitoa hukumu ya kesi iliyokuwa imefikishwa mbele yake na aliyekuwa mgombea wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Bi. Hawa Ng'umbi, akipiga matokeo yaliyompa ushindi Mbunge wa Jimbo la Ubungo,Bw. John Mnyika.

Hukumu hiyo ilisomwa na jaji Bi. Upendo Msuya, na  kubainisha kuwa mdai katika kesi hiyo ameshindwa kuithibitishia mahakama pasipo kuacha shaka juu ya madai aliyokuwa akiyalalamikia.  Kesi ya kupinga matokea
zisifunguliwe kwa jazba



Jaji Msuya alisema kuwa katika madai hayo ushahidi wa mashahidi wa mdai haukuwa na nguvu na kwamba mdai hakuleta mashahidi wa kuunga mkono madai  yake.

Hii ni moja kati ya kesi nyingi ambazo zimefunguliwa na baadhi ya wabunge wakipinga matokeo dhidi ya wapinzani hao. Tunakumbuka wakati uchaguzi ulipomalizika aliyekuwa Katibu Mkuu wa CCM, Bw. Yusuf Makamba, aliwataka wagombea wote wa chama hicho walioshindwa kufungua kesi za kupinga matokeo kwa ahadi kuwa chama kitawasaidia.

Ahadi hiyo ya Bw. Makamba inatufanya tuamini kuwa iliwafanya baadhi ya wagombea wa chama hicho walioshindwa kufungua kesi hata kama hawakuwa na ushahidi wa kutosha.

Japokuwa ni haki yao ya msingi kufanya hivyo,lakini kesi zinazotupiliwa mbali na mahakama zinatakiwa kuwa ushahidi kwetu kuwa baadhi yao walifungua kesi kwa shinikizo, bila ushahidi wa kutosha.

Mfano mzuri ni kama kesi hiyo ambayo hukumu iliyotolewa jana. Kesi kama hizi mara nyingi zinafunguliwa kwa jazba bila watu kutafakari,

Kwa msingi huo tunaiomba Serikali sasa ifikiri upya namna ambavyo inaweza kutunga sheria itakayosaidia kuwabana watu wanaokimbilia mahakamani kufungua kesi baada ya kushinda bila kuwa na ushahidi wa kutosha.

Tunasema hivyo kwa kutambua kuwa Serikali inatumia fedha nyingi kuendesha kesi za aina hiyo. Wote tunakumbuka kuwa kuna wakati mahakama ilikwama kusikiliza kesi hizo kutokana na uhaba wa fedha, lakini baada ya mahakama kulalamika ilitoa fungu hilo ili zianze kusikilizwa.

Lakini baadhi ya kesi zinaonekana hazikuwa na kichwa wala miguu, matokeo yake zimesababisha fedha za walipa kodi kupote, ambapo zingetumika kwa ajili shughuli zingine za maendeleo.

Tunatoa mwito itungwe sheria yenye meno makali itakayosaidia kuwabana wanaoshindwa na kukimbilia mahakamani bila kuwa na ushahidi wa kile wanachokidai. Kwa kufanya hivyo tutaokoa fedha za wananchi zinazotumika kuendesha kesi hizo.

No comments:

Post a Comment