23 December 2011

Hamad Rashid akanusha kuomba radhi

*Asema Maalim Seif anakabiliwa na mashtaka manne
*Akusudia kumshtaki kwa Lipumba achukuliwe hatua


Na Benedict Kaguo, Tanga

MBUNGE wa Wawi, Zanzibar, Bw.Hamad Rashid Mohamed, amesema anakusudia kuwasilisha mashtaka manne dhidi ya Katibu Mkuu wa chama
hicho, Maalim Seif Sharif Hamad ambaye pia ni Makamu wa Kwanza wa Rais wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa Zanzibar kwa madai ya kushindwa kusimamia shughuli za chama.

Bw.Mohamed anatarajia kuwasilisha mashtaka hayo kesho kwa Mwenyekiti wa chama hicho Taifa, Profesa Ibrahim Lipumba na kueleza jinsi Maalim Seif ilivyoshindwa kusimamia majukumu yake na kusababisha chama hicho kupoteza mwelekeo.

Akizungumza na waandishi wa habari mjini Tanga jana, Bw.Mohamed alikanusha taarifa zilizochapishwa na gazeti moja linalotoka kila siku siyo (Majira) likimnukuu kuwa amekwenda kuomba radhi kwa Maalim Seif ili asifutiwe uanachama na kupoteza ubunge kama yaliyomkuta Mbunge wa Kigoma Kusini, Bw.David Kafulila.

Bw.Mohamed alisema, anashangazwa na Maalim Seif kuendeleza malumbano katika vyombo vya habari na kukiuka agizo lake kuwa matatizo yote yanayohusu chama hicho yafikishwe katika vikao vya chama si vinginevyo.

“Kimsingi mimi sijamuomba radhi Maalim Seif kama ilivyoripotiwa na gazeti moja linalotoka kila siku, hadi sasa bado sijawasilisha rasmi mashtaka yanayomkabili kwa maandishi badala yake nimekuwa nikiona habari tofauti zikitoka katika vyombo vya habari na kudai nimeomba radhi jambo ambalo si kweli.

“Hakuna mashtaka yoyote niliyoletewa mimi binafsi wala wenzangu zaidi ya kusikia wenzetu wanafanya vikao vya kutushambulia kwamba sisi ni wasaliti na tumepewa pesa na Waziri Mkuu, Bw.Mizengo Pinda ili kudhoofisha chama,” alisema.

Aliongeza kuwa, dhamira yao ni kupeleka mashtaka manne kwa Prof.Lipumba wakimtuhumu Maalim Seif ili hatua ziweze kuchukuliwa.

Aliyataja mashtaka hayo kuwa ni pamoja na ofisi yake kushindwa kufanya kazi za chama upande wa bara na kusababisha chama hicho kishindwe vibaya katika Uchaguzi Mkuu mwaka 2010.

Dai lingine ni matumizi mabaya ya fedha na rasilimali za chama ambapo shtaka la tatu ni ofisi yake kushindwa kutoa huduma stahiki kwa upande wa Bara na Zanzibar.

Alisema programu iliyopitishwa na Baraza Kuu la chama hicho ya kutembelea wanachama, ilikuwa ianze Januari 2012 lakini kuna baadhi ya viongozi wameanza kupita visiwani kabla ya muda.

Bw.Mohamed alisema shtaka la nne ni chama hicho kushindwa kuutendea haki upande mmoja wa Jamhuri akitolea mfano katika Uchaguzi Mkuu uliopita, Maalim Seif alishindwa kushiriki katika uzinduzi na ufungaji wa kampeni kwa upande wa bara.

“Haya ndiyo madai ya msingi hivyo ningependa kuona chama kikiyajibu ili kuleta mustakabali mzuri, kama yatashindwa kujibiwa nitachukua hatua ya kwenda kwa wananchi kuwaeleza kilichotokea,” alisema.

Katika hatua nyingine, Bw.Mohamed alisema alifuatwa na Mashekhe wawili akiwemo Shekhe Abdalah Saleh ili kumtaka atafute suluhu badala ya kuendeleza mgogoro ndani ya chama.

“Ushauri wao niliukubali na ndiyo sera ya chama chetu ambacho kinaelekeza kuwa, migogoro inayojitokeza itamalizwa ndani ya chama ili kulinda heshima ya chama, kudumisha amani na utulivu wa nchi,” alisema Bw.Mohamed.






6 comments:

  1. Maadam imdekua hivyo CUF imedpotza dira

    ReplyDelete
  2. Hamad Rashid uroho wa madaraka unakusumbua sasa kama unanguvu muondowe katibu mkuu aliepo ili ukae wewe kubali upepo wa mageuzi unapokuja usitegemee kila siku utakuwa juu pia shukuru ukiteremka kama una nia ya kugombea subiri mwaka 2014 hauko mbali hata kama unataka urais ni haki yako lakini hebu subiri. Pia kwanini hayo matamshi yako unayotowa kwa nini huyatowi jimboni kwako na wale ndio walikufanya uwe na jeuri hiyo.

    ReplyDelete
  3. wacha walaluane Mume wao CCM yupo kimya

    ReplyDelete
  4. Nd. Hamadi rashid, unafanya siasa za kizamani, unaropokwa tu, wewe tulikuona mtu wa maana mwenye busara unafaa kuchukua uongozi katika ngazi za juu katika nchi hii, leo unaropokwa tu, sababu unataka madaraka kwa pupa. unajifanya unajua sana kumbe mbele kiza. Tushakupiga mhuri hufaii tena, rabda uanzishe chama chako wewe na waroho wenzako. hivi ivyo viopesa vya ruzuku ndo vinmakutoeni roho. Tunajua ulizoea raha wakati ulipokua kiongozi Bungeni, sheikh kila ktu kinamuda wake. wako umepta.

    ReplyDelete
  5. Hamad rudi wawi,unasema Maalim Hakufanya hata kampeni moja Bara sasa hawa kina Lipumba walikua na kazi gani,au ndo wewe umekua mtetezi wa wa bara mpaka kwenu umesahau hata kujenga,huoni aibu umejiimarisha bara wawi hata kibanda cha kujifichia mvua huna.Ama kweli unazeeka vibaya

    ReplyDelete
  6. Bw.Mohamed alisema, "anashangazwa na Maalim Seif kuendeleza malumbano katika vyombo vya habari na kukiuka agizo lake kuwa matatizo yote yanayohusu chama hicho yafikishwe katika vikao vya chama si vinginevyo"

    Mbona hatujamsikia huyo Maalim kuendeleza malumbano kwa njia hiyo ya vyombao vya habari. Siku zote tunakusia wewe tuu ukilalamika. mtu mzima haitwi muongo lakini wewe HRM uanitwa kizabizabina

    ReplyDelete