01 December 2010

Guardiola awapongeza wachezaji wake

MADRID, Hispania

KOCHA wa Barcelona, Pep Guardiola amewapongeza wachezaji wake kwa kucheza kwa kujituma na kuibuka na ushindi wa mabao 5-0, dhidi ya Real Madrid 5-0.Mechi hiyo
maarufu kama 'El Clasico' iliyochezwa Jumatatu Hispania inakadiriwa kuangaliwa na watu milioni 400, katika televisheni duniani.

Kinyume na matarajio ya kuona soka ya ushindani zaidi, Barca ikiwa katika uwanja wake wa Camp Nou, iliwasasambua Real Madrid mabao 5-0.

Matokeo hayo ni mabaya zaidi kwa Jose Mourinho, katika Ligi Kuu ya Hispania akiwa na Real Madrid msimu huu.

Guardiola, ambaye ameiwezesha timu yake kuibuka na ushindi kwa mara ya tano dhidi ya Madrid, tangu aanze kuinoa, aliwapongeza wachezaji wake kwa kuweza kuonesha Dunia uchezaji wao wa soka ya kushambulia.

"Tunajivunia kwa kuwa dunia imetuona tukicheza namna ambayo tunapenda kucheza," Guardiola alisema.

"Tumefanya, inatufanya sisi kujivuna. Sasa acha tukae na kufurahia ushindi, tutaangalia mchezo mzima, itakuwa kitu kibaya kama hatutaendelea kushinda. Mchezo kama ule hutokea kwa nadra sana."

Licha ya kuonekana kuimiliki Real, Guardiola alisema mbio za kuwania ubingwa bado zipo.

"Bado kuna mechi nyingi zimebakia kucheza katika ligi hii," alisema.

"Tulikuwa ni timu nzuri sana usiku wa leo (Juzi), timu zote ziko katika kiwango cha juu. Tuko juu kwa pointi mbili zaidi (33) mbele ya Real (31) na Real ni timu nzuri."

"Ningependa kuchukua pointi zaidi kutoka kwa Madrid, lakini haiwezekani. Timu ile ina nguvu zote, iko nyuma kwa pointi mbili tu, lakini tumeridhika."

Kabla ya mechi ya juzi, Real ndiyo ilikuwa ikiongoza ligi kwenye msimamo.

No comments:

Post a Comment