22 October 2013

JK AMLILIA NYAISANGA, KUAGWA LEO LEADERS’ CLUB



  Rais Jakaya Kikwete, amemtumia salamu za rambirambi katika kuomboleza kifo cha mtangazaji mkongwe nchini aliyekuwa Meneja wa Kituo cha Abood Media, Julius Nyaisanga kwa jina maarufu Uncle J, anaripoti Mwandishi Wetu.

  Nyaisanga ambaye aliwahi kufanya kazi Radio Tanzania Dar es Salaam (RTD) kwa sasa TBC Taifa na Kampuni ya IPP Media ambako alikuwa Mkurugenzi wa Radio One, alifariki dunia Oktoba 20 mwaka huu, mkoani Morogoro. kwa ugonjwa wa kisukari.
  “Nimeshtushwa, nimesikitishwa na kuhuzunishwa kwa kifo cha mtangazaji maarufu na mkongwe nchini katika tasnia ya habari hususan upande wa utangazaji.
 “Julius Nyaisanga ameacha pengo kubwa katika tasnia hii, enzi ya uhai wake alikuwa na bidii kubwa ya kazi na mwenye sauti iliyokuwa na mvuto mkubwa kwa wasikilizaji,” alisema.
  Rais Kikwete alitoa pole kwa familia ya marehemu kwa kuondokewa na kiongozi wa familia na kuwahakikishia wanafamilia, ndugu na jamaa zake kuwa yuko pamoja nao katika kuomboleza msiba huo.
  Alitoa pole kwa waandishi wa habari na watangazaji kote nchini kwa kumpoteza mwanataaluma mwenzao ambaye kuondoka kwake kumesababisha pengo kubwa katika taaluma ya habari na utangazaji nchini.
  Wakti huo huo, mwili wa marehemu Nyaisanga leo utaagwa katika Viwanja vya Leaders Club, Kinondoni, Dar es Salaam kuazia saa nne asubuhi na baadaye kusafirishwa kwenda nyumbani kwao Tarime, mkoani Mara kwa mazishi.
  Taarifa iliyotolewa na Jukwaa la Wahariri nchini (TEF), ilisema Nyaisanga ni miongoni mwa wanahabari ambao wajumbe wa jukwaa kila walipofika Morogoro kwa shughuli mbalimbali, walishirikiana naye ndani na nje ya mikutano.
  TEF itamkumbuka daima jinsi alivyoweka alama yake katika tasnia ya habari ambapo alama hizo zitaendelea kuwa hai kuenziwa kwa kutekeleza wajibu na maadili ya taaluma.
.

No comments:

Post a Comment