12 August 2013

WAFUASI WA SHEKHE PONDA WATINGA MAHAKAMA KUU



 Na Rehema Mohamed
WAFUASI 52 wa Shekhe P o n d a I s s a P o n d a , waliohukumiwa adhabu ya kifungo cha mwaka mmoja jela, wamekata rufaa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, wakipinga hukumu ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu iliyowatia hatiani.

Katika rufaa yao hiyo, wafungwa hao, kupitia kwa wakili wao, Mohamed Tibanyendela, wanapinga hukumu ya Mahakama ya Kisutu, ambapo pamoja na mambo mengine, wanadai kuwa hakimu alikosea kisheria kuchambua ushahidi wa pande zote uliowasilishwa mahakamani hapo.
Pia wanadai kuwa katika hukumu hiyo, hakimu alijikanganya kwa kumwachia huru mmoja wa washtakiwa na kuwatia hatiani washtakiwa wengine.
Ru f a a h i y o ime p a n gwa kusikilizwa leo na Jaji Salvatory Bongole, mahakamani hapo. Machi mwaka huu Hakimu Sundi Fimbo wa Mahakama ya Kisutu aliwahukumu washtakiwa hao wa kesi ya kula njama na kufanya maandamano isivyo halali kwenda jela mwaka mmoja baada ya kuwatia hatiani katika mkosa yaliyokuwa yakiwakabili.
Washtakiwa hao walidaiwa kutenda makosa hayo Februari 15, mwaka huu. Washtakiwa katika kesi hiyo walikuwa ni Salum Makame, Said Idd na Ally Nandumbi, Makame, Idd na Nandumbi, Hussein Athumani, Seif Rwambo, Abdull Ally, Waziri Swed, Naziru Waziri, Ahmad Rashid, Jumanne Kayogola, Hamis Tita, Amri Diyaga, Salum Said, Rajabu Mpita na Haji Sheluhenda, Abdul Ahmed, Bakari Mwambele, Ramadhani Fadhili na Awadh Juma.
Wengine ni Omari Mkwau, Kassim Chobo, Abubakari Bakari, Ramadhani Milambo, Hamis Ndeka, Athuman Juma, Abdallah Salum, Juma Makoti, Bashir Kakatu, Imam Omari, Rashid Lukuta, Bakari Athumani, Mbwana Kassim, Nurdin Ahmed, Mustapha Mide, Rajabu Kifumbo, Zuberi Juma.
Wengine ni Omari Mkandi, Idrisa Katulimo, Sawali Mola, Said Dudu, Ramadhani Juma, Mussa Sinde, Issa Sobo, Yahaya Salum, Jabil Twahil, Shomari Tarimo, Hashim Bendera, Waziri Toy, Athuman Yahaya, Yasin Seleman, Shaban Malenda, Yasin Mohamed, Khatib Abdallah na Rajabu Rashid wote wakazi wa jijini Dar es Salaam.
Awali, ilidaiwa kuwa katika siku ya tukio, wilaya ya Ilala, jijini Dar es Salaam, washtakiwa wote kwa pamoja walikula njama za kufanya maandamano isivyo halali.
Shtaka la pili, ilidaiwa kuwa siku na eneo la tukio la kwanza, washtakiwa walifanya mkusanyiko usio halali kwa lengo la kusababisha uvunjifu wa amani.
Shtaka la tatu ilidaiwa kuwa washtakiwa wote kwa pamoja walikiuka amri ya Jeshi la Polisi ya kutoa zuio la kufanya maandamano na kufanya mkusanyiko ulisababisha vurugu na uvunjifu wa amani.
Katika shtaka la nne, ilidaiwa kuwa mshtakiwa Makame, Idd na Nandumbi, waliwashawishi wananchi kwa kuwasambazia vipeperushi vya kuhamasisha kufanya maandamano yasiyo halali.

No comments:

Post a Comment