13 January 2012

WANANCHI wa Jimbo la Newala mkoani Mtwara

Na Rachel Balama

WANANCHI wa Jimbo la Newala mkoani Mtwara  wameomba kupatiwa elimu kuhusu ununuzi wa hisa ili wapate ufahamu na kuweza kununua hisa hizo kutoka katika benki ya Wananchi wa Newala iliyoanzishwa hivi karibuni.
Wakizungumza na mwandishi wa majira Dar es salaama jana wananchi hao ambao hawakupenda majina yao kuchapishwa gezetini, walisema kuwa  Mbunge wa Jimbo hilo ambaye pia ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa(TAMISEMI) Bw. George Mkuchika amekuwa akiwahamasisha wananchi hao kununu hisa katika benki hiyo wakati wananchi hao hawana uelewa kuhusu hisa.

"Bw. Mkuchika ambaye ni mhasisi wa benki hiyo amekuwa akituhamasisha kununua hisa za benki hiyo lakini asilimia kubwa ya wananchi huku hatujui maana ya hisa," alisema mwannchi mmmoja wa Newala.

Wananchi hao wamemuomba Mbunge huyo  kuitisha mkutano na kuwashirikisha wananchi pamoja na wadau mbalimbali ili kuelezena hali halisi kuhusu maendeleo ya jimbo hilo.

Waliongeza kuwa itakuwa ni vyema mkutano huo ukafanyika wilayani Newala na si Dar es Salaam ili kutoa nafasi kwa wananchi hao kujadili mustakabali mzima wa Jimbo lao.

Waliongeza kuwa ni hatua nzuri ya kuanzishwa kwa benki hiyo ya Wananchi wa Newala lakini wananchi hao wanapaswa kupewa elimu kuhusu hisa ili waweze kununua hisa nyingi na kuongeza mapato kwenye benki hiyo.

Walisema kuwa haitaleta maana kuanzisha benki ya wananchi harafu viongozi wahamasishe wananchi kununua hisa wakati hawana uelewa.

Mwisho

Na Mwandishi Wetu, Lindi

ALIYEWAHI  kuwa Mbunge wa Jimbo la Mchinga  mkoani  Lindi, Bw. Mudhihili  Mudhihili, ametoa  msaada wa vifaa mbalimbali, zikiwemo kompyuta kwa Shule ya  Sekondari Mchinga zenye thamani ya sh.milioni 10 milioni ili kuinua  kiwango cha elimu.

Msaada huo uliokabidhiwa juzi kwa  uongozi wa Shule hiyo  ni pamoja na kompyuta tano,Photocopy mashine moja na Printer  moja, ikiwa ni moja ya sehemu ya msaada wake katika kuchangia maendeleo ya elimu Jimboni humo.

Akikabidhi vifaa hivyo, Bw. Mudhihili alisema ameamua kutoa msaada huo, ikiwa ni sehemu ya majukumu yake katika kuchangia maendeleo  ya kata, Tarafa na Jimbo kwa ajili ya kuinua kiwango cha elimu kwa watoto ambao ni tegemeo kubwa kwa Taifa letu.

Bw. Mudhihili ambaye aliwahi kushikilia Jimbo hilo kwa kipindi cha miaka 15 mfululizo,alisema amefanya hivyo kutokana na yeye wakati akiwa Mbunge, alikuwa mstari wa mbele kuwahimiza wananchi kuchangia maendeleo yao yakiwemo ya elimu, badala ya kuitegemea Serikali pekee kwa kila jambo.


“Sasa na mimi nimekuwa mkazi wa Mchinga na sio kiongozi, hivyo ni wajibu wangu kutekeleza yale niliyokuwa nina wahimiza wenzangu” alisema Bw.Mudhihili.

Amewataka wananchi wote wa wilaya ya Lindi  kuondoa mawazo potofu kutoka vichwani mwao kwamba misaada anayoitoa ina lenga kutaka kuwania nafasi hiyo ya ubunge kwa mara nyingine mwaka 2012.

Mbunge huyo wa zamani aliuchekesha umma uliokuwa umeudhuria hafla ya kukabidhi kompyuta hizo, pale aliposema kule Bungeni hakuna kitu alichokisahau ikiwemo peni au kitambaa cha leso, huku akimtaka mbunge wa sasa Bw. Said Mtanda kuendelea kufanya kazi ya kuwatumikia wananchi kwa amani na utulivu bila ya hofu dhidi yake.

Alisema  msaada huo  ni mwanzo na kwamba kila atakapofanikiwa kupata wafadhili atahakikisha anaipeleka kwenye Jimbo hilo kwa manufaa na maendeleo ya watoto wakiwemo wa wakulima na masikini wanaosoma katika shule za jimbo hilo ikiwemo ya Mchinga.

Kwa upande wake  mjumbe wa Bodi ya  shule hiyo Bw.  Ally Salum, alimshukuru Bw. Mudhihili kwa moyo wa uzalendo aliouonyesha wa kuipatia shule hiyo msaada huo wa kompyuta.

1 comment:

  1. Hakika suala la kuanzisha bank ya wananchi wa Newala ni zuri sana ila linanitatiza. Kwanza ni ushirikishwaji wa wananchi. Mchakato wa kwanza ulitakiwa uwe maoni ya wananchi. Je, wanasemaje kuhusu kuanzishwa bank? Je, nini kifanyike? Pili, sijapenda hili ya kukata hela kwa lazima kwenye kila kilo ya korosho kuchangia uanzishaji wa bank hiyo, tena wakulima wenyewe wamekopwa. Wakati Mbunge alipoitisha kikao kuongea na wananchi wa Newala waishio Dar es Salaam kilichofanyika Msimbazi centre alikuja na maamuzi yake na watu wake. Alidai kuwa wananchi wameshirikishwa, hii sio kweli. Akumbuke kuwa mwaka 2015 upo karibu. Watanzania wa sasa sio wale wa mwaka 1945. Wameamka. Wanataka viongozi walio wakweli, wenye uchungu nao.

    Kwa Maoni yangu mimi ni kwamba Mfuko wa Maendeleo ya Newala(NDF) ungefufuliwa na huo ndio ungezaa bank ya wananchi. Tatizo ni kwamba kuna wabunge hawataki kushauriwa na iwapo utasema ukweli unachukiwa. Namuelewa vizuri kaka yangu George Huruma Mkuchika na naomba jambo hili alifanyie kazi. Aitishe kikao cha kuongea na wananchi kule kwenye jimbo lake aangalie hili la kuifufua NDF na bank itokane na NDF. Akumbuke shule za sekondari zilizopatikana kutokana na NDF.

    ReplyDelete