20 December 2011

TBF kumpa tuzo Jaji Ramadhan

Na Amina Athumani

SHIRIKISHO la Mpira wa Kikapu Tanzania (TBF), linatarajia kutoa tuzo ya heshima kwa viongozi waliouletea mafanikio mchezo huo akiwemo
Jaji Mkuu Mstaafu, Augustino Ramadhani.

Akizungumza kwa simu, Dar es Salaam jana Rais wa TBF, Mussa Mzia alisema tuzo hizo ilikuwa zitolewe katika hafla ya kukabidhi zawadi za washindi wa michuano ya Taifa 'Taifa Cup', lakini hawakufanya hivyo.

"Tunajipanga zaidi kwa sababu ni wengi waliotoa mchango mkubwa katika mchezo huu wa kikapu, mmoja wao akiwa ni mlezi wetu Jaji Ramadhan," alisema Mzia.

Alisema utaratibu huo utafanyika na wataangalia majina ya viongozi na wadau walioleta mafanikio hayo katika kipindi cha miaka 50 iliyopita ya Uhuru wa Tanzania Bara.

Mzia alisema kwa sasa watapendekeza majina ya watu 15 au 20, watakaopatiwa tuzo na wakikamilisha watatangaza siku ya hafla.

No comments:

Post a Comment