06 June 2011

Polisi watakiwa kuondoa utata wa mauaji

Na Moses Mabula, Tabora

JESHI la Polisi mkoani Tabora limetakiwa kufanya uchunguzi wa kina kuhusiana na tukio la kuuawa kwa mwanamke na kisha kutundikwa juu ya dari kwa lengo la
kupotosha sababu za mauaji hayo.

Hatua hiyo imeombwa na baadhi ya wananchi na wakazi wa kitongoji cha Miseto,kijiji cha Kamama, wilayani Uyui ambao wanapinga taarifa ya mauaji hayo.

Wakazi hao walidai kuwa mwanamke aliyeuawa anayejulikana kwa jina la Nyamizi Mhoja (30) na anayedaiwa kumfanyia kitendo hicho ni Ali Mayoe (35) wote wakazi wa kijiji cha Kamama wilayani humo.

Wakizungumza na Majira kwa sharti la kutotajwa majina yao wananchi hao walisema tukio la kuuawa kwa mawanamke huyo lilitokea Aprili 22 mwaka huu baada ya kuzuka mabishano kati yao kuhusiana na kuhama walipokuwa wakiishi.

Walisema kuwa wamefikia hatua ya kueleza hayo kwenye vyombo vya habari ili wananchi na wapenda haki wajue jinsi lilivyotokea ambapo watendaji wanalifumbia macho sakata hilo pamoja na kuwa kuwa wazi.

Aidha wananchi hao waliongeza kuwa hata katika mkutano wa hadhara uliofanywa na mbunge wa Igalula Dkt. Athuman Mfutakamba baadhi ya wananchi walitamka hadharani kuwa baadhi ya watendaji wanamkumbatia muuaji baada ya kupiga mkewe hadi kufa.

"Tulisema wazi siku alipokuja mbunge wetu kuwa watendaji hao hawafai waondolewe....wameficha mauaji ya mwanamke aliyepigwa wakashiriki kutunga uongo kuwa alijinyonga wakati sisi tunajua kulizuka ugomvi kabla ya mauti hayajamkuta mwanamke huyo" walisema.

No comments:

Post a Comment