06 December 2010

'Usiku wa Club E Vegas' wanaoga Dar

Na Mwandishi Wetu

MASHABIKI wa muziki jijini Dar es Salaam, mwishoni mwa wiki walipata burudani ya aina yake katika Ukumbi wa Mlimani City, ambapo bendi za Malaika ya Afrika Kusini na African Stars 'Twanga Pepeta' ziliweza kutoa uhondo wa nguvu kwenye 'Usiku wa
Club E Vegas 2010'.

Licha ya bendi hizo kuwashika mashabiki katika ukumbi huo pia kulikuwa na makundi ya Wanne Star na Baucha, ambayo yalo yalikuwa kivutio kwa mashabiki waliofika ukumbini hapo kutokana na wasanii wake walivyokuwa makini jukwaani.

Katika usiku huo mashabiki hao, walipata kila walichopenda kwenye shoo kabambe zilizovurumishwa na waburudishaji mahiri katika tukio ambalo lililovuta watu wengi na kukutanisha watu wa aina tofauti.

Baadhi ya wageni walipata fursa ya kupiga picha na warembo ambao walikuwa wamejipanga pembeni mwa gari la aina ya limousine lililopamba lango la Ukumbi wa Mlimani City.

Licha ya burudani ya nguvu kutolewa katika ukumbi huo, mashabiki pia waliweza kucheza michezo mbalimbali ikiwemo kamari, gurudumu la bahati, ndoa chap chap, kula, kunywa na wengine wakicheza kuendana na mipigo mbalimbali iliyokuwa ikiporomoshwa.

Kabla ya saa mbili jioni, kundi la wasichana, wakiwa wamevaa nguo nyekundu waliingia na kuonesha ubunifu wa mavazi wa aina yake pamoja na kucheza dansi.

Naye Wane Star aliingia na kundi lake la ngoma za jadi na kuburudisha kwa dakika 30, huku wasanii wake wakiwa  wamevailia za Kiafrika.
Bendi ya Malaika liingia jukwaani na kibao chake kilichokuwa na mchanganyiko wa Afro pop kikiwekwa vionjo vya kijadi vya kwaito, soul, mbaqanga, pop-rock na dansi yenyewe ya kawaida sasa.

Hatimaye usiku wa saa sita iliingia bendi ya African Stars, kwa mtindo wa aina yake, huku wanenguaji wake 16 wakivutana.

Club E yenye wanachama zaidi ya 2000, ilianza mwaka 2007 na imekuwa ikiandaa hafla sehemu mbalimbali nchini mwaka mzima, huku kilele chake kikiwa ni Dar es Salaam kila Desemba.

No comments:

Post a Comment