28 December 2010

Mtoto wa miezi mitano aibwa Temeke

Na Leah Kassopa

MWANAMKE mmoja asiyefahamika aliiba mtoto wa miezi mitano, Twaha Masudi katika eneo la Mtoni Relini Wilaya ya Temeke, Desemba, 26 mwaka huu.Kamanda wa Mkoa wa Kipolisi Temeke, Bw. David Misime alisema
taarifa ilitolewa na mama wa mtoto aliyeibwa, Bi. Fatuma Hamisi 'Mama Twaha' (30) kuwa mwanamke huyo asiyefahamika alifika nyumbani kwa mama huyo siku ya Krismasi akiulizia  chumba cha kupanga.

"Mama Twaha alimjibu chumba kipo, hivyo akalipa sh. 50,000 za pango na kuondoka huku akiahidi kurudi siku iliyofuata, yaani Desemba 26, mwaka huu," alisema Bw. Misime.

Siku iliyoafuata mwanamke huyo alirudi bila vyombo vyake na kumuuliza Mama Twaha amuelekeze dukani ili kununua mahitaji madogo madogo, kisha 'mpangaji' huyo mpya alipoomba aende na mtoto huyo dukani, na alipoondoka hakurudi tena. Upelelezi wa kumtafuta mtuhumiwa na mtoto bado uanendelea.

No comments:

Post a Comment