25 November 2010

Yanga yanywea kwa Manji.

*Sendeu avunjwa nguvu.

Na Elizabeth Mayemba

KAMATI ya Utendaji ya Yanga, imekubaliana na mapendekezo ya Mdhamini wake, Yusuf Manji na kuahidi kuanza kuyafanyia kazi haraka na pia imeamuliwa kuanzia sasa Msemaji wa
klabu hiyo, atakuwa ni Mwenyekiti na Katibu Mkuu.

Katika kikao hicho cha Kamati ya Utendaji, viongozi hao walikitumia kwa ajili ya kufuta tofauti zao zilizojitokeza hivi karibuni na kuombana radhi.

Awali mdhamini huyo, alitoa mapendekezo kwa uongozi likiwemo kuhakiki mapato na matumizi, kutibiwa kwa mchezaji Shamte Ally na Wajumbe wa Kamati ya Utendaji kutafutiwa semina maalumu katika Chuo cha Usimamizi wa Fedha kwa lengo la kujinoa katika masuala ya kibiashara.

Akizungumza Dar es Salaam jana Mwenyekiti wa klabu hiyo, Lloyd Nchunga alisema katika kikao Kamati ya Utendaji kilichokutana juzi pamoja na Manji walikubaliana mambo mbalimbali kwa ajili ya maendeleo ya klabu hiyo.

"Tumejadili mambo mengi na mjadala ukawa mrefu yakiwemo ya usajili, rasilimali za klabu, uongozi, bodi ya udhamini, na pia tulifuta tofauti zetu pande zote mbili na kuombana msamaha," alisema Nchunga.

Alisema katika la ukaguzi, kamati yake itaweka hadharani ripoti ya mapato na matumizi ya klabu na imekubalika kuwa ukaguzi wa mahesabu uliokuwa ukiendelea ukamilishwe na atafutwe mkaguzi wa mahesabu kutoka nje ili wafanye ukaguzi maalumu kwa kipindi cha miezi mitatu, walichokaa madarakani na matokeo ya awali ya ukaguzi yatajulishwa kwa wanachama katika kipindi cha siku sitini.

"Ili kujenga uwezo wa kutekeleza mipango ya maendeleo iliyokusudiwa, tumekubaliana kwamba wajumbe wa Kamati ya Utendaji, watafute semina maalumu katika Chuo cha Usimamizi wa Fedha kwa lengo la kujinoa kwenye masuala ya kibiashara," alisema.

Akizungumzia suala la usemaji wa habari za Yanga ambazo zinatakiwa kufanywa na Ofisa Habari wake, Louis Sendeu, Nchunga alisema endapo mtu atataka kuzungumza jambo lolote kwa niaba ya klabu, ni lazima apate idhini ya maandishi kutoka kwa Mwenyekiti.

Alisema Sendeu ataendelea kuwa msemaji, lakini baada ya kupata idhini ya maandishi kutoka kwa Katibu Mkuu, hivyo uongozi utachukua hatua kali kwa yeyote atakayekiuka utaratibu huo.

2 comments:

  1. pETRO eUSEBIUS mSELEWANovember 25, 2010 at 10:13 AM

    Money is honey...can cure,protect,injure and kill.

    ReplyDelete
  2. Mimi naona yanga msijipendekeze kwa Manji eti kisa pesa. Yanga imekuwepo hata kabla ya Uhuru Manji kitu gani? Pili yanga sio timu ya CCM mnatuboa sana kuihusisha yanga na CCM au kama vipi badilisheni malengo ya klabu na muwe chama cha siasa

    ReplyDelete