Na Mwandishi Wetu
Baraza la Wanawake la Chama cha Demokrasia na Maendeleo (BAWACHA), limeitaka serikali kupitia Wizara ya Habari, Utamaduni, Vijana na Michezo kuingilia kati suala la mchezaji wa timu ya taifa ya wanawake (Twiga Stars), Sophia Mwasikili ambaye amekwenda nchini Uturuki kucheza soka la kulipwa katika Klabu ya Luleburgazgucu Spor Kulubu.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari jana na Katibu wa BAWACHA, Mwakyoma Kaihula ilieleza kwamba kuna uzembe katika kutuma Hati ya Uhamisho wa Kimataifa (ITC) ya mchezaji huyo katika klabu yake mpya, ambayo inapaswa kutolewa na Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF).
Kaihula alisema baraza lake limekuwa likifuatilia kwa karibu maendeleo ya Sophia ambaye ni nahodha wa Twiga Stars, tangu alipoitwa kujiunga na Luleburgazgucu Spor Kulubu ya nchini Uturuki, kucheza soka la kulipwa.
"Ni ukweli ulio wazi kwamba hizo zilikuwa ni habari njema kwa maendeleo ya soka ya nchi yetu na kwa hakika zilitia moyo kwa vijana wa kike, ambao wangependa kupata ajira na kujenga maisha yao kupitia nyanja ya michezo.
"Kwa jinsi ambavyo habari hizo zilivyopokelewa, kisha zikahanikiza anga ya tasnia ya michezo Tanzania, zimedhihirisha namna ambavyo Watanzania, wapenda michezo wako tayari kutoa ushirikiano kwa wachezaji wao wa ndani, kila wanapopata nafasi ya kwenda kucheza soka la kulipwa nje ya nchi," alisema.
Alisema hii inadhihirisha pia kuwa Watanzania wamechoka kushabikia wanasoka wa nchi zingine za Afrika, ambazo kutokana na mipango na sera nzuri zinazopangwa na serikali zao, wamefanikiwa kusakata soka nje ya mipaka ya nchi zao.
Katibu huyo alisema kwa bahati mbaya, tangu habari hizi za kukwama kwa Sopfhia, zianze kusikika, TFF hawajatoa maelezo ya kina. Hali ambayo imeruhusu wadau mbalimbali wa suala hili kujadili na kutoa hitimisho kadri wanavyoweza.
Jana baadhi ya vyombo vya habari viliripoti kwamba ITC ya nahodha huyo wa Twiga Stars, bado haijatumwa nchini Uturuki hali ambayo ina muweka njia panda mchezaji huyo.
No comments:
Post a Comment