17 February 2011

Mtoto anaswa na umeme Dar

Na Nassra Abulla

MTOTO aliyetambulika kwa jina la Amina Ahmed (7) amekufa papo hapo jana baada ya kunaswa na umeme katika Mtaa wa Sunna, Magomeni
jijini Dar es salaam.

Amina akiwa na wenzake walienda nyumba ya jirani ambaye jina lake halikufahamika majira ya saa 7:00 mchana kwa lengo la kusoma, ghafla alishika bomba la antena ya televisheni iliyokuwa imegusana na umeme na kunaswa.

Akizungumza na waandishi wa habari juzi, Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kinondoni, Bw. Charles Kenyela alisema maiti imehifadhiwa katika Hospitali ya Mwanayamala.

Wakati huohuo maiti ya mtu mmoja aliteyetambulika kwa jina la Desmund Mtenga (42) imekutwa chumbani kwake katika eneo la Kinondoni block namba 41.

Bw. Kenyela alisema maiti hiyo ilikutwa chumbani imelala kifudifudi majira ya saa 3:00 asubuhi ikiwa haina jeraha lolote, na chanzo cha kifo bado kinachunguzwa.

Uchunguzi wa awali unaonesha kuwa marehemu enzi za uhai wake alikuwa na tabia ya kunywa pombe kali/konyagi, maiti imehifadhiwa katika hospitali ya Mwananyamala na uchunguzi unaendelea.

No comments:

Post a Comment